Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na Rais Mstaafu wa Afrika Kusini Mhe. Thabo Mbeki ambapo viongozi hao wawili wamezungumzia masuala mbalimbali kuhusu Umoja wa Afrika (AU).

Pamoja na kuzungumzia masuala yahusuyo Umoja wa Afrika, Rais Mstaafu Thabo Mbeki amempongeza Rais Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Rais Mstaafu Thabo Mbeki pia amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi kubwa alizozifanya katika uongozi wa nchi kwa kipindi cha mwaka mmoja aliomo madarakani.
Kwa upande wake Rais Magufuli amemshukuru Rais Mstaafu Thabo Mbeki kwa kumtembelea na kufanya nae mazungumzo na pia amempongeza kwa kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Usomi na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.