MFANYABIASHARA maarufu wa Jijini Arusha mwenye asili ya kiasia, Firoz Khane (55) amesomewa mashitaka yake ya awali katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha kwa kosa la kuhujumu uchumi na kulisababishia taifa hasara ya zaidi ya Sh milioni 657.5
Khane amesomewa mashitaka ya awali ya uhujumu uchumi. 

Mbele ya Hakimu Mfawidhi Mkoa wa Arusha, Agustino Rwizile imedaiwa kuwa mshitakiwa huyo kati ya mwaka 2013 na mwaka 2014, alisababisha hasara kwa kuingiza mitambo ya mawasiliano na kutoza gharama za kimataifa kinyume cha sheria.
Pia mshitakiwa anadaiwa kusajili majina ya kughushi, kuuza mashine za mawasiliano na kumiliki mtambo wa mawasiliano huku akitumia mawasiliano ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) bila idhini ya serikali kujipatia mamilioni ya fedha.
Mshitakiwa huyo amekana mashitaka. Mahakama imemnyima dhamana kwa kuwa mashitaka hayo hayana dhamana.
Kesi hiyo itasikilizwa tena Desemba 16. Upande wa serikali unatarajiwa kulwa na mashahidi kuthibitisha madai yanayomkabili mshitakiwa huyo.