Mwanamuziki mashuhuri nchini Marekani Janet Jackson amejifungua mtoto wa kiume akiwa na umri wa miaka 50, afisa wake wa mawasiliano amethibitisha.
Taarifa imesema mwanamuziki huyo na mumewe Wissam Al Mana, ambaye ni mfanyabiashara kutoka Qatar, wana furaha kumpata mtoto wa kiume kwa jina Eissa Al Mana.
"Janet alijifungua bila matatizo yoyote na kwa sasa anapumzika," afisa wake amesema.Watu walianza kushuku kuwa alikuwa ameshika mimba Aprili mwaka jana alipoahirisha ziara yake ya kutumbuiza ya Unbreakable.
Alipakia video kwenye Twitter wakati huo na kuwaambia mashabiki kwamba alikuwa anaahirisha ziara hiyo "kwa sababu kulitokea mabadiliko ya ghafla".
Janet Jackson akitumbuiza London mwaka 2011Image copyrightREUTERS
Image captionJanet Jackson akitumbuiza London mwaka 2011
"Nilifikiri ni muhimu sana kwenu kuwa wa kwanza kufahamu hili," alisema, na kuongeza: "Tafadhali, naomba mjaribu kunielewa kwamba ni muhimu sana nilifanye hili kwa sasa."
Alisema alitaka kuangazia kuunga familia na mumewe, ambaye walifunga pingu za maisha mwaka 2012.
Jackson alikuwa awali ameonekana akinunua nguo na vitu vingine vya kutumiwa na watoto London.

Wasifu: Janet Jackson
Janet Jackson arrives for the premiere of Why Did I Get Married Too? at the Brixton Ritzy cinema, London (May 2010)Image copyrightPA
  • Janet Damita Jo Jackson alizaliwa 16 Mei 1966 mjini Gary, Indiana
  • Ndiye kitinda mimba miongoni mwa watoto tisa familia yake na ni dadake nyota wa muziki wa Pop marehemu Michael Jackson
  • Alichomoa albamu yake ya kwanza, Janet Jackson, mwaka 1982
  • Ana jumla ya albamu11 ya karibuni zaidi, Unbreakable, akiichomoa 2015
  • Ameshinda tuzo za Grammy mara saba
  • Alianza kwa kuigiza kipindi cha maisha ya uhalisia cha familia kwenye runinga cha The Jacksons mwaka 1976. Ameigiza katika filamu kadha ikiwemo ya Tyler Perry ya Why Did I Get Married
  • Kwa sasa anaishi na mumewe wa tatu, bilionea wa Qatar Wissam al-Mana, waliyefunga naye ndoa 2012
  • Ndoa zake za awali ni ya mwaka mmoja na mwanamuziki wa soul James DeBarge imiaka ya 1980 na kwa mcheza densi Rene Elizondo Jr kuanzia 1991-2000

Janet Jackson ndiye mtu mashuhuri pekee aliyejifungua mtoto akiwa na umri mkubwa.
Mshindi wa tuzo ya Oscar Halle Berry alijaliwa mtoto wake wa pili akiwa na miaka 47 miaka mitatu iliyopita.
Na mke wa John Travolta, Kelly Preston, alijifungua mtoto wake wa tatu akiwa na miaka 48.
Nchini India hata hivyo, kuna wanawake watatu ambao wamedaiwa kujifungua watoto wakiwa na zaidi ya miaka 70.
Janet JacketImage copyrightJANET JACKSON/@TWITTER
Image captionJanet Jackson alitangaza angeahirisha ziara yake Aprili ili kuangazia kujenga familia