Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Songea, Damian Dallu
MAASKOFU wa makanisa mbalimbali nchini, wamesema unyenyekevu wa viongozi wa serikali, uadilifu na uwajibikaji na kusimamia misingi ya upendo na umoja hasa kwa wanyonge, vitaisogeza Tanzania kwenye neema mwaka 2017.
Aidha viongozi hao wa dini wamewahimiza Watanzania kuwaombea viongozi walioko madarakani, kuombea amani na kuziombea sera za nchi hasa ya viwanda, ili Mungu awezeshe mipango mizuri kwa nchi itekelezeke mwaka huu.

Aidha wametaka taifa kukabiliana na biashara haramu ya dawa za kulevya kwa kuwakamata waliowaita tembo wa dawa hizo badala ya watumiaji.
Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Songea, Damian Dallu akihubiri juzi katika Ibada ya Misa Takatifu ya mkesha wa mwaka mpya katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Mathias Mulumba Kalemba, aliwakumbusha viongozi na watendaji wa serikali nchini kuliongoza Taifa, kwa misingi ya haki, unyenyekevu, na upendo kwa wananchi wa kawaida.
Askofu Dallu alisema unyenyekevu na upendo huo utawezesha haki kutenda kwa wananchi hatua itakayosaidia kudumisha amani, mshikamano na nchi kupiga hatua za maendeleo zaidi mwaka huu.
Alisema yapo mataifa yameingia katika machafuko kutokana na viongozi wake kushindwa kutumia hekima na busara, katika kutatua changamoto na migogoro mbalimbali inayowakabili wananchi wake wanaowaongoza na kutaka viongozi wa Tanzania kudumisha umoja na kuongoza kwa upendo.
Dallu pia alilaani vitendo vya kuwakatili watu wenye ualbino kwa kukata viungo vyao ili kupata utajiri na kukemea wanasiasa wenye tabia hiyo kuacha mara moja na kumhofu Mungu.
Kwa upande wake, Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa amewaasa watanzania kuombea amani ya dunia kwani maovu ni mengi, ikiwemo maadili kupotea na kusababisha watu kuoneshwa katika televisheni wakitembea nusu uchi bila hofu.
Ngalalekumtwa ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki la Iringa, alisema hayo jana alipokuwa akihubiri katika misa ya mwaka mpya katika Kanisa la Moyo Mtakatifu wa Yesu, Kihesa, Iringa. Misa hiyo iliyorushwa moja kwa moja na kituo cha Radio Maria na Radio Tumaini.
Alisema ukitaka kujua maovu yamekuwa mengi ni kupitia vituo vya televisheni ambapo utaona vipindi vinavyooneshwa ni vile visivyokuwa na maadili ikiwa ni pamoja na kuonesha watu waliovaa nusu uchi.
“Kwa kweli tuombee amani ya dunia hii, maovu yamekuwa mengi mno, ukitaka kujua hilo wewe fungulia televisheni yako tu utaona, watu wanapigana ngumi, vipindi vinavyooneshwa ni watu wamevaa nusu uchi na wengine wako uchi kabisa,” alisema Ngalalekumtwa.
Aidha alisema uovu mwingine ni pamoja na vijana wanatafuta fedha za haraka haraka na pia matumizi ya dawa za kulevya huku wanaokamatwa wakiwa ni watumiaji badala ya wale wanaoingiza nchini ambao amewaita kuwa ni tembo.
Ngalalekumtwa aliwataka watu kuyasahau mambo yote mabaya ya mwaka uliopita lakini yasaidie kutoa mafunzo katika kutenda mambo mema mwaka huu mpya na pia miaka ijayo.
Alisema, “Mambo yote ya mwaka jana yawe shule kwetu sisi, tusipojifunza kwa mambo ya mwaka jana hatutajua mwaka huu tufanyeje na yale mazuri tuyaboreshe na mabaya tuyakwepe,” alisema Ngalalekumtwa.
Aliwaasa pia watu kujiuliza mienendo ya maisha yao na kuacha uvivu, uchoyo, ugomvi na mambo yote mabaya wamwachie shetani aondoke nayo Alisema Mungu huwapa binadamu bila hata ya kuomba lakini ni vizuri zaidi kumuomba wakati wote ambapo aliwaasa kumuomba Mungu mvua za kutosha na chakula.
Kwa upande wake, Kanisa la Moravian, Jimbo la Mashariki na Pwani Tanzania limewasihi viongozi wote wa dini kuunga mkono jitihada za maendeleo za Rais John Magufuli na serikali yake kwa kuongeza bidii katika kufundisha maadili mema kwa vijana na watoto.
Katibu Mkuu wa Kanisa la Moravian Jimbo la Mashariki na Pwani Tanzania, Askofu Emmaus Mwamakula aliyasema hayo wakati akitoa salamu za mwaka mpya za kanisa hilo.
“Wakati Rais na Serikali yake wanaweka mkazo katika kujenga na kuweka miundombinu ya kiuchumi kwa kujenga viwanda, barabara na reli sisi kama Kanisa na viongozi wa dini kwa ujumla tuunge mkono jitihada hizo,” alisema.
Huko Dodoma, Watanzania wametakiwa kuiombea Sera ya Viwanda iliyoletwa na Serikali ya Awamu ya Tano iweze kufanikiwa ili kupunguza tatizo la ajira nchini. Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Askofu wa Kanda ya Kati wa Kanisa la Pentecostal Holiness Association Mission Tanzania (PHAMT), Julius Bundala kwenye ibada ya kuukaribisha mwaka mpya 2017.
Ibada ilifanyika katika kanisa hilo lililopo Chinyoya, mkoani Dodoma. Askofu Bundala alisema vijana wengi wa kitanzania wapo mtaani wakizurura kutokana na kukosa ajira hivyo ni wajibu wa Watanzania kufanya maombi ili sera ya viwanda iweze kufanikiwa.
Alisema sera ya Tanzania ya viwanda ikifanikiwa vijana wanaozurura mtaani wataacha na hivyo kukuza uchumi.
Aidha Askofu Bundala alibariki mwaka 2017 akimuomba Mungu aibariki nchi na watu wake. Vile vile aliwataka Watanzania kutenda matendo mema ya kimaendeleo ya kumpendeza Mungu katika mwaka 2017 na kuachana na tabia za kuiga mambo yasiyokuwa na tija kama vile ulevi na uasherati.
Pia aliwataka wazazi na walezi kusomesha watoto wao ili kuepukana na tabia ya watoto kuzagaa mitaani na kuwa ombaomba.
Askofu Bundala aliwataka kutumia mwanya wa serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli ya elimu bure, ili kuwasomeshe watoto na kufanya hivyo kutaondoa tatizo la ombaomba Mkoani hapa.
Shehe wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa Salum alisema Serikali ya Rais John Magufuli imerejesha nidhamu kwa watumishi wa umma na kuwataka Watanzania waiunge mkono kwa kulipa kodi ili maendeleo yapatikane mwaka huu.
Shehe Salum alisema jana akizungumza na gazeti hili kwa simu kuwa, nidhamu iliyopo kwa watendaji hivi sasa nchini inatakiwa pia kuhamia kwa Watanzania, kwanza kufanyakazi kwa bidii na kuwa wazalendo kwa nchi yao.
“Tunashukuru Mungu ametuvusha salama mwaka 2016 na tumeingia mwaka 2017, tunapaswa kuangalia mwelekeo wa Rais na Serikali yake iliyopo madarakani nasi twende nao huo mwelekeo, tufanye kazi kwa bidii. Uzalendo wa kweli ni kulipa kodi, ukilipa kodi unaonesha kweli unaijali nchi yako,” alisisitiza Shehe Salum.
Alisema mwelekeo ulivyo unaonesha Tanzania inakwenda kujitegemea kimapato lakini kama watanzania hawatalipa kodi, maendeleo na kujitegemea huko hakutaonekana na tutazidi kutegemea wafadhali jambo alilosema si lenye afya.
Imeandikwa na Hellen Mlacky na Regina Kumba, Dar es Salaam, Muhidin Amri, Songea na Sifa Lubasi, Dodoma.