Mkurugenzi wa Bohari ya Dawa (MSD) Laurean Bwanakunu (kushoto), akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, wakati akitoa taarifa ya kuimarika kwa upatikanaji wa dawa nchini. Kulia ni Ofisa Mwandamizi wa Idara Habari Maelezo, Zamaradi Kawawa.

Na Dotto Mwaibale

MKURUGENZI wa Bohari ya Dawa (MSD) Laurean Bwanakunu amesema hali ya upatikanaji wa dawa kwasasa imeboreshwa kutoka asilimia 54 iliyokuwepo mwaka jana, hadi kufikia asilimia 74 hivi sasa. 

Ameuhakikishia umma uwa upatikanaji wa dawa utaimarika mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu hadi kufikia asilimia 90.

Amesema kwa sasa kati ya aina za dawa muhimu 135 zinazohitajika kuwepo MSD dawa aina 100 zinapatika kwenye maghala ya MSD

Mkurugenzi wa MSD, Bwanakunu ameyasema hayo mbele ya waandishi wa habari, Dar es Salaam leo Ukumbi wa Idara ya habari Maelezo, alipokuwa kwenye mkutano ulioandaliwa na idara katika jukumu lake la kutoa nafasi kwa Idara na Taasisi za serikali kuelezea utekelezaji wa majukumu yao.

Katika hatua nyingine, Bwanakunu ameeleza kuwa, MSD imefanikiwa kurejesha Maghala iliyokuwa imekodi kwa ajili ya kuhifadhia vifaa tiba, hatua ambayo inaokoa sh.Bilioni 4 ambazo zilikuwa zikilipwa kama kodi kila mwaka. 

Ameongeza kuwa, tayari wamekabidhiwa kiwanja eneo la Luguruni, wilayani Ubungo walichopewa na Rais John Magufuli ambacho kitatumika kujenga ofisi za Kanda ya Dar es Salaam.

Kuhusu maduka, ameeleza kuwa wiki ijayo wanatarajia kuzindua  duka la dawa la MSD mkoani Katavi, ambalo litaifanya MSD kuwa na jumla ya maduka Saba, mengine yakiwa mkoani Arusha, Dar es Salaam, Mwanza, Lindi, Geita naMbeya. 

Akijibu swali juu ya ukosefu wa vifaa vyakujifungulia wajawazito Mkurugenzi Mkuu amesema vipo vyakutosha,na  zabuni ya manunuzi ya vifungashio kwa ajili ya vifaa hivyo vyakujifungulia iko katika mchakato wa kumpata mshitiri. 

Ameeleza kuwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu anaangalia namna ya kuwawezesha akina mama wasio kuwa na uwezo wakununua vifaa hivyo ambapo
utaratibu huo atautoa baadae.

Kwa sasa MSD inanunua dawa na vifaa tiba moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji, ilikuhakikisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba unakuwaendelevu na kupunguza gharama za ununuzi wa dawa hizo, ambazo asilimia 80 zinatoka nje ya nchi.