Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita (RAS), Selestine Gesimba akizungumza na wataalamu wa kilimo kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech), Jukwaa la Bioteknojia na Uhandisi Jeni (OFAB) pamoja na wanahabari walipofika ofisini kwake wakiwa katika ziara ya kutoa mafunzo ya kilimo chenye tija kwa maofisa ugani wa mkoa huo leo.


Mtaalamu wa masuala ya mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ukiliguru jijini Mwanza, Dk. Jeremiah Simon akitoa maelezo kwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita (RAS), Selestine Gesimba kabla ya kuanza ziara ya mafunzo hayo.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita (RAS), Selestine Gesimba akiwaonesha shamba la mfano la mahindi ambalo lipo nje ya ofisi yake wataalamu hao wa kilimo pamoja na wanahabari (hawapo pichani). Kulia ni Mshauri wa Jukwaa la Kilimo na Bioteknojia (OFAB), Dk.Nicholaus Nyange na kushoto ni Mratibu wa Jukwaa hilo Tanzania, Philbert Nyinondi.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita (RAS), Selestine Gesimba akionesha shamba la mfano la alizeti ambalo lipo nje ya ofisi yake. Kushoto ni  Mratibu wa Jukwaa hilo Tanzania, Philbert Nyinondi.

Zao la alizeti likioneshwa.
Ofisa Program wa OFAB kutoka Shirika la AATF, Suleiman Okoth (wa nne kutoka kulia), akiwa na wataalamu hao wakilimo wakati wakiangalia bwawa la samaki la mfano lililopo nje ya ofisi ya mkuu wa mkoa wa Geita.
Ofisa Uvuvi wa Mkoa wa Geita, Tito Mlelwa akiwa mbele ya bwala la samaki la mfano lililopo nje ya ofisi ya mkuu wa mkoa huo huo wakati akizungumza na wanahabari.
Jengo la Ofisi la Halmshauri ya Wilaya ya Chato linavyoonekana.
Maofisa Ugani wa Halmshauri ya Wilaya ya Chato wakiwa kwenye mafunzo ya kilimo chenye tija.
Ofisa Ugani kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, David Makabila (kulia) akizungumza kabla ya kuanza kwa mafunzo hayo.
Maofisa Ugani wakifuatilia mada katika mafunzo hayo.
Maofisa Ugani wakiandika wakati wa mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmshauri ya Wilaya ya Chato, Martin Ndilanha (kulia), akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea. Kutoka kulia ni Ofisa Program wa OFAB kutoka Shirika la AATF, Suleiman Okoth, Ofisa Ugani wa Wilaya ya Chato, Charles Ntaki na Mratibu wa OFAB Tanzania, Philbert Nyinondi.
Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Chato, Elias Makory akifungua mafunzo hayo.
Mshauri wa Jukwaa la Kilimo na Bioteknojia (OFAB), Dk.Nicholaus Nyange (kulia), akitoa mada katika mafunzo ya kilimo ya siku moja kwa maofisa ugani wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita leo ambayo yameratibiwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech), kupitia Jukwaa hilo. 

Mtaalamu wa masuala ya mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ukiliguru jijini Mwanza, Dk. Jeremiah Simon akitoa mada katika mafunzo hayo.


Na Dotto Mwaibale, Chato


MAOFISA Ugani wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita wameombwa kuwa weredi zaidi katika masuala ya kilimo ili elimu waliyonayo waweze kuitoa kwa wakulima ili nao waweze kulima kilimo chenye tija cha zao la mihogo ili zao hilo liweze kukubalika katika soko la kimataifa.


Mwito huo umetolewa na Mtaalamu wa masuala ya mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ukiliguru jijini Mwanza, Dk. Jeremiah Simon wakati akitoa mafunzo kwa maofisa Ugani wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita leo ambayo yameandaliwa na Tume ya Sayansi ya Teknolojia (Costech) kupitia Jukwaa la Wazi la Bioteknolojia kwa manufaa ya kilimo (OFAB). 


Alisema hivi sasa nchi ya China na Tanzania zimesaini  mkataba wa ununuzi wa zao la muhogo jambo ambalo ni fursa kwa wakulima wetu wa hapa nchini wakiwemo wa kutoka wilaya ya Chato.

"Hii ni fursa kubwa kiuchumi lakini ni vema sasa tukaingia katika kilimo chenye tija ili mihogo yetu iweze kuingia katika soko la kimataifa badala ya kuendelea na kilimo kisicho na tija" alisema Simon.

Katika kuonyesha kuwa swala la kilimo na shuguli za ugani ni muhimu katika kusaidia kuboresha kilimo na kuongeza tija kwa wakulima katibu tawala wa mkoa wa Geita,  Selestine Gesimba ameanzisha mashamba darasa ya mfano ya mazao mbalimbali nje ya ofisi yake.

Amesema lengo la kufanya hivyo nje ya ofisi yake ni kuonyesha kwa vitendo dhana nzima ya ugani kwani anaamini mkulima anaamini akiona kwa macho yake kuliko kusikia.

Hata hivyo amesema kila halmashauri itatakiwa kuwa na mashamba madogo ya mfano kwenye ofisi zao kuonyesha kilimo bora cha mazao muhimu kwenye wilaya pamoja na ufugaji bora wa mifugo na samaki.

Katibu tawala huyo wa mkoa wa Geita amesema kwa kufanya hivyo kuanzia mkoani wilayani na kwenye kata na vijiji kwa kusimamiwa na wataalamu wa mazao na mifugo wakulima watajifunza na tija itaonekana.

Nje ya ofisi hiyo ya katibu tawala wa mkoa na mkuu wa mkoa wa Geita wameweka vishamba vidogo vya mahindi, Alizeti, Maharage pamoja na bwawa la kufugia samaki ambalo wananchi watakwenda kujifunza lakini wanajiandaa kuweka na mifugo mingine kama ng'ombe,kuku na mifugo mingine.

Akiwasilisha mada yake juu ya kilimo bora cha zao la pamba mtafiti na mtaalamu wa magonjwa ya mazao kutoka kituo cha utafiti wa kilimo Ukiliguru Stellah Chirimi amewataka maafisa Ugani hao kushauri wakulima kila mtu kuwa na ekari moja ya Pamba iliyolimwa na kuhudumiwa kisasa ili kupata tija.

Amesema wakulima wengi hawazingatii kilimo bora cha kupanda kwa mstari ili kuwa na idadi inayotakiwa ya miche kwenye shamba na kujikuta wanalima ekari nyingi ambazo hazina matunzo kabisa hali ambayo inawapekea kupata mavuno yasiyo na tija.

Amesisitiza umuhimu wa kila Ofisa Ugani kuwa na mashamba madogo ya mfano kwenye kata zao ambayo wakulima watakwenda kuona na kujifuza kuliko kutumia mashamba ya wakulima pekee.