Mwanajeshi wa Marekani ameuawa wakati wa operesheni ya kukabiliana na wanamgambo wa al-Shabab, jeshi la Marekani limesema.
Mwanajeshi huyo aliuawa Alhamisi umbali wa takriban kilomita 64 magharibi mwa mji mkuu Mogadishu, katika mji wa Barii.

Wanajeshi wa Marekani walikuwa wanawashauri na kuwasaidia wanajeshi wa Jeshi la Taifa la Marekani wakati wa operesheni hiyo, jeshi la Marekani limesema.
Shirika la habari la Reuters limeripoti kuwa wanajeshi wengine wawili wa Marekani walijeruhiwa kwenye mapigano.
"Mwanajeshi huyo alipigwa risasi alipokuwa kwenye operesheni ya kushauri na kusaidia Jeshi la Taifa la Somalia. Wanajeshi wawili walijeruhiwa katika kisa hicho. Wawili hao wanapokea matibabu," msemaji wa jeshi la Marekani Afrika (Africom) Robyn Mack ameambia AFP.
Rais wa Marekani Donald Trump aliongeza majukumu ya kijeshi la jeshi la Marekani dhidi ya al-Shabab majuzi na kuwapa fursa ya kushiriki kwenye operesheni dhidi ya wanamgambo hao wa mtandao wa al-Qaeda.
Kuuawa kwa Mmarekani huo kumetokea siku tatu pekee tangu mkuu mpya wa jopo kazi la Marekani la kuangazia eneo la upembe wa Afrika Brigidia Jenerali David J. Furness kuzuru Mogadishu.
Alisema "tumejitolea kufanya kazi na mataifa washirika kuisaidia Somalia kusimama kidete dhidi ya kundi hili la msimamo mkali."
Mwaka 1993, wanajeshi wa Marekani walipokuwa wanashiriki kijeshi Somalia, wanajeshi 18 waliuawa mjini Mogadishu wakipigana na wanamgambo wa kiukoo.
Kisa hicho kiliangaziwa katika kitabu na filamu ya 'Black Hawk
Down'.
Al-Shabab wamekuwa wakipigana dhidi ya serikali ya taifa ya Somalia ambayo inaungwa mkono na jamii ya kimataifa.