Meneja wa Jukwaa la Bioteknolojia Afrika (OFAB), Daniel Otunge, akizungumza wakati akitoa mada kwenye semina ya siku tatu iliyowakutanisha wanahabari na watafiti wa kilimo kutoka nchi tano za Afrika Uganda, Kenya, Burknafaso, Ethiopia na Tanzania ambayo ilikuwa mwenyeji wa semina hiyo iliyoanza juzi jijini Mwanza.


 Watoa mada wakijiandaa. 


 Mtafiti Mkuu wa Jukwaa la Bioteknolojia Tanzania (OFAB),Dk. Emmarold Mneney akitoa mada kwenye semina hiyo.
 Usikivu katika semina hiyo.
 Maswali yakiulizwa kwenye semina hiyo.
 Wanahabari wakiwa kwenye semina hiyo. 
 Mratibu wa Jukwaa la Bioteknolojia Tanzania (OFAB), Filbert Nyinondi (kushoto),akiteta jambo na Meneja wa Jukwaa la Bioteknolojia Afrika (OFAB), Daniel Otunge wakati wa muda wa mapumziko.


 Mshauri Mkuu wa Mradi wa Utafiti wa Mahindi Yanayostahimili Ukame Afrika (WEMA) Tawi la Tanzania Dk.Alois Kulaya akitoa mada.
 Mratibu wa Jukwaa la Bioteknojia kutoka nchini Uganda, Philip Chemonges, akitoa mada.
 Mtaalamu wa masuala ya kilimo kutoka  Nairobi nchini Kenya, Paul Chege akitoa mada.
Mtafiti wa kilimo kutoka Ethiopia, Dk.Endale akitoa mada.
Washiriki wa Semina hiyo na watoa mada wakiwa katika picha ya pamoja.


Na Dotto Mwaibale, Mwanza

NCHI za Afrika zimetakiwa kuwekeza kwenye kilimo kwa kuwa
kilimo ni biashara na chakula.

Mwito huo umetolewa na Mratibu wa Jukwaa la Bioteknojia
kutoka nchini Uganda, Philip Chemonges jijini Mwanza jana wakati akitoa mada
kwenye semina ya siku tatu iliyowakutanisha wanahabari na watafiti wa kilimo
kutoka nchi tano za Afrika Uganda, Kenya, Burknafaso, Ethiopia na Tanzania
ambayo ilikuwa mwenyeji wa semina hiyo.

"Hivi sasa kilimo ni muhimu hivyo ni vizuri nchi za
Afrika ziamke na kuwekeza katika kilimo kwani kilimo ni biashara na
kinatukomboa kwa chakula" alisema Chemonges.

Katika hatua nyingine Meneja wa Jukwaa la Bioteknolojia
Afrika (OFAB), Daniel Otunge amewataka waandishi kutoka nchi hizo kushirikiana
na wataalamu wa kilimo ili kupata fursa ya kuandika habari za kilimo kwa
ufasaha pasipo kuwepo  upotoshaji.


Otunge alisema lengo la semina hiyo iliyoandaliwa na Jukwaa
la Bioteknolojia Afrika (OFAB) kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti na
Maendeleo kwa ajili ya Manufaa ya Wakulima Wadogo (AATF) ni kuwakutanisha
waandishi wa habari na wataalamu wa kilimo waweze kukutana na kupeana uzoefu wa
jinsi ya kuandika habari za kilimo cha Bioteknolojia kwa ufanisi.

Alisema wakati wote wamekuwa wakihitaji kilimo cha kisasa
ambacho kinafanyika kisayansi ili kiweze kumsaidia mkulima kutumia mbegu bora
zenye uwezo wa kukinzana na wadudu na magonjwa na zile zinazostahimili ukame.

Alisema changamoto kubwa iliyopo hivi sasa ni kushindwa
kuanza kwa matumizi ya bioteknojia baada ya watafiti kufanya utafiti ambao
umekuwa ukisubiri kuruhusiwa na nchi husika.

Mtaalamu wa masuala ya kilimo kutoka Nairobi nchini Kenya, Paul
Chege alisema teknolojia hiyo mpya ya kilimo ambayo inafanyika katika nchi tatu
za Afrika Kusini, Sudan na Burknafaso ambayo imesimama kwa kuwa wanashughulikia
nyuzi za pamba imewasaidia wakulima mazao yao yasishambuliwe na wadudu kwani
mimea yake yenyewe inakuwa na kinga.



Mshauri Mkuu wa Mradi wa Utafiti wa Mahindi Yanayostahimili
Ukame Afrika (WEMA) Tawi la Tanzania Dk.Alois Kulaya alisema muhimu kilimo
kifanyike kwa kutumia bioteknolojia kwa kuzalisha mbegu badala ya kuendelea na
matumizi ya kilimo cha zamani ambacho hakina tija.

Alishuri kuendeleza kilimo cha matumizi ya teknolojia za
uhandisi jeni (GMO), kwani kina tija kwa wakulima baada ya kuonesha mafanikio
kwa baadhi ya nchi kama ya Burknafaso kwenye kilimo cha  pamba.

Mtafiti Mkuu wa Jukwaa la Bioteknolojia Tanzania (OFAB),Dk.
Emmarold Mneney alisema wakati ufike nchi iwekeze kwa kuongeza watafiti wa
kutosha ili kusaidia wakulima katika kilimo chenye tija.



(Imeandaliwa na mtandao wa www.habari za jamii.com-simu namba 0712-727062)