Jackline Ngalo ambaye ni Mwanasheria wa shirika la kutetea Haki za watoto wafanyakazi wa nyumbani nchini, WOTESAWA, akizungumza na Lake Fm, baada ya semina kwa viongozi wa serikali za Kata/Mitaa pamoja na wadau wengine wa maendeleo katika wilaya za Ilemela na Nyamagana mkoani Mwanza ili kuwajengea uwezo wa kutetea haki za watoto wafanyakazi wa nyumbani katika maeneo yao.

Na Binagi Media Group
Semina kwa viongozi wa serikali za Mitaa pamoja na wadau wengine wa maendeleo katika wilaya za Ilemela na Nyamagana mkoani Mwanza ikiendelea Jijini Mwanza
Semina hiyo imeandaliwa na shirika la WOTESAWA kwa siku tatu tangu Mei 09 hadi leo Mei 11,2017
Washiriki wa semina hiyo wakimsikiliza mwanahabari Nashon Kenedy, wakati akichangia mada kwenye semina hiyo
Wadau wa Maendeleo mkoani Mwanza wameidhinisha mikakati mbalimbali ikiwemo kufanya sensa ya watoto wafanyakazi wa nyumbani na utungwaji wa sheria ndogo ndogo za kuwalinda watoto, lengo likiwa ni kusaidia mapambano dhidi ya ukatili kwa watoto hao.

Wamefikia makubaliano hayo leo kwenye kilele cha mafunzo ya siku tatu kwa viongozi wa serikali za mitaa kutoka Wilaya za Nyamagana na Ilemela yaliyoandaliwa na Shirika la kutetea Haki za watoto wafanyakazi wa nyumbani la WOTESAWA lililopo Jijini Mwanza.

Akizungumzia mikakati hiyo, Jackline Ngalo ambaye ni Mwanasheria wa shirika la WOTESAWA amebainisha kwamba, mikakati hiyo itasaidia kuwalinda watoto wafanyakazi wa nyumbani ikiwemo kuwanusuru na utumikishwaji wa kazi nzito huku wakilipwa ujira mdogo.

Wadau walioafiki mikakati hiyo ni Madiwani, Watendaji wa Kata, Wenyeviti wa Mitaa, Maafisa Ustawi na Maendeleo ya Jamii ambapo wameongeza kwamba mafunzo hayo yatawasaidia kuielimisha jamii kupitia mikutano ya hadhara ili kuepukana na ukatili kwa watoto hususani wafanyakazi wa nyumbani.

Baadhi ya watoto wamekuwa wakikosa fursa ya kusoma kutokana na kuajiriwa katika kazi za nyumbani kinyume na sheria huku wakilipwa ujira mdogo tofauti na waraka wamishahara wa mwaka 2013 unavyoelekeza.

Waraka huo unaelekeza kwamba mfanyakazi wa kazi za nyumbani anapaswa kulipwa kiwango cha chini cha mshahara ambacho ni shingili 150,000 iwapo mwajiri ni balozi ama mfanyabiashara mkubwa, elfu 80,000 ikiwa mwajiriwa haishi kwenye nyumba ya mwajiri wake, elfu 40,000 ikiwa mwajiriwa anaishi kwenye nyumba ya mwajiri wake na shilingi 130,000 ikiwa mwajiri ni raia wa kigeni. Tazama picha zaidi hapa