Polisi katika mji wa Portland nchini Marekani, wanasema wanaume wawili waliuawa, walipojaribu kumzuia mwanamume aliyewatukana kiubaguzi, wanawake wawili, walioonekana kuwa Waislamu.
Kisa hicho kilitokea kwenye treni jana.

Polisi wanasema mwanamume aliyekuwa akitukana, aliwageukia wanaume hao waliojaribu kuingilia kati, na kuwadunga visu na kuwauwa.
Abiria mwengine alijeruhiwa, kabla ya mshambuliaji kukamatwa.
Halmashauri ya uhusiano baina ya Marekani na Waislamu, imesema Rais Trump lazima atoe kauli kulaani chuki inayozidi dhidi ya Waislamu.
Imesema hali inazidi kuwa mbaya kwa sababu ya maneno ya rais na sera zake.