Zoezi la kuhesabu kura limeanza nchini Burundi baada ya kura ya maoni iliyopigwa kwa amani kwa kiasi kikubwa kubadili katiba ya nchi na kupanua mipaka ya muda wa Rais.

Vituo vingi vya kupigia kura vimeripoti mwitikio wa wapiga kura kwa kiasi kikubwa, ingawa upinzani wanadai vijana wa chama tawala waliwashinikiza baadhi ya wapiga kura kwenye vituo vya kupigia kura.Wakosoaji na wafuatiliaji wa siasa za Burundi wanadai kuwa Rais Pierre Nkurunziza anatumia katiba kushika hatamu za uongozi .
Karatasi za kupigia kura zilikuwa na maneno mawili tu yalyomuongoza mpiga kura kuchagua NDIYO ama HAPANA.Wapiga kura walitakiwa kupitisha mabadiliko ya katiba ili kutoa nafasi ya uraisi kusalia madarakani kwa miaka mitano hadi saba.
Raisi Nkurunziza ameridhishwa na mwitikio wa wapiga kura katika vituo vya kupigia kura na kuita kuwa ni ishara ya uzalendo mkubwa .
Ingawa mpinzani wake mkuu aliyeko nchini Burundi , Agathon Rwasa, alikuwa na madai kuwa baadhi ya wapiga kura walilazimishwa kupiga kura, na wengine kupigwa na hata kukamatwa katika maeneo ya nje ya mji mkuu Bujumbura.
Katiba mpya, endapo itapitishwa, itamruhusu raisi Nkurunziza kugombea mihula miwili zaidi, na kumpa nafasi ya kusalia madarakani kwa miaka kumi na minne zaidi.
Viongozi wa upinzani walioko uhamishoni wameonya juu ya kura kama hiyo na kubainisha kuwa itaua makubaliano ya amani yaliyosababisha yeye kuingia madarakani mara ya kwanza.
Muda wa Rais wa sasa unamalizika mwaka wa 2020, lakini ikiwa atafanikiwa kwenye kura ya maoni anaweza kutawala mpaka 2034.