Waziri wa uhamiaji wa Denmark ameshutumiwa vikali kutokana na pendekezo lake kuwa Waislamu wawe wanachukua mapumziko wakati wa mwezi wa Ramadhani kwa sababu ya alichodai kuwa usalama wa jamii nzima.

Inger Stojberg, ambaye amekuwa akifahamika kwa kutekeleza sera kali za uhamiaji, amesema kufunga saa za kazi siku nzima kunaleta changamoto kikazi.
Amedai kuwa kunaweza kusababisha hatari hasa kwa waendesha mabasi ya abiria na wafanyakazi wa hospitalini kufanya kazi muda mrefu bila kula.
Makampuni ya mabasi yalikuwa ya kwanza kusema kuwa hawana shida na Waislamu kuendelea na kazi wakati wa mwezi wa Ramadhani.
Kampuni ya mabasi ya Ariva inayofanya safari zake nchini Denmark, imesema hawajawahi kupata ajali iliyowahusisha madereva waliofunga.
''Suala hilo sio tatizo kwetu'' alieleza msemaji wa Ariva, Hammershoy Splittorff alipozungumza na gazeti la Berlingske Tidende.
Ujumbe kama huo ulitoka kwa chama cha wafanyakazi wa sekta ya usafirishaji, ambacho kiongozi wake Jan Villadsen alionesha mashaka kuwa waziri alikuwa analitengeneza tatizo ambalo halipo kabisa.
Umoja wa Waislamu nchini humo waliandika kwenye mitandao ya kijamii wakimshutumu waziri huyo, na kumweleza kuwa Waislamu ni watu wazima ambao wanaweza kujichunga wenyewe na jamii kwa ujumla hata kama wakifunga.
Waziri Stojberg amekosolewa huku wanasiasa wakitakiwa kutatua matatizo ya kweli na si kuingilia.
Waislamu duniani kote wako kwenye mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani
Image captionWaislamu duniani kote wako kwenye mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani
Waziri alisemaje?
Inger Stojberg aliandika mawazo yake kuwa Denmark ina uhuru wa kuabudu na kuwa dini ni suala binafsi.
Lakini aliwataka Waislamu wanaofunga mwezi wa Ramadhani nchini humo kutofanya kazi kwa kuwa wakati mwingine wanahitajika kufanya kazi kwa saa nyingi , kazi ambazo zinahusisha pia kushika mashine hatari.
Alitoa mfano wa madereva wa mabasi ambao hawali wala kula kwa zaidi ya saa kumi na kusema kuwa kufunga kunaweza kuathiri usalama na uwezo wao wa uzalishaji
''Natoa wito kwa Waislamu kuchukua likizo wakati wa mwezi wa Ramadhani kuepuka madhara kwa jamii nzima ya Denmark.