Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Aboubakar Kunenge, leo Ijumaa, Oktoba 2, 2020, amezindua safari ya kwanza ya treni ya abiria kutoka Dar es Salaam kwenda mkoani Arusha iliyokuwa imekosekana kwa takribani miaka 30 na kusababisha adha ya usafiri kwa wananchi.

Akizindua safari hiyo RC Kunenge amelielekeza Shirika la Reli Tanzania TRC kuhakikisha wanaendelea kutoa huduma Bora za usafiri na kuwapongeza Kwa mapinduzi makubwa na mazuri wanayoyafanya kwenye usafiri wa reli.

Aidha RC Kunenge amesema treni hiyo itasaidia wafanyabiashara na wananchi hususani wa kipato cha kawaida kupata usafiri wa haraka na kwa bei nafuu hivyo ametoa wito kwa wananchi kuchangamkia fursa hiyo.

Pamoja na hayo RC Kunenge ameipongeza serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli kwa kutekeleza kwa vitendo ahadi alizotoa na maamuzi yake ya kufufua usafiri wa treni.

Kwa upande wake Mkurugwnzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania TRC, Eng. Masanja Kadogosa amesema Shirika hilo limejidhatiti vyema kuhakikisha linatoa huduma bora na salama kwa wananchi wote.