Mbeya. Viongozi wa vyama vya Siasa na wananchi jijini Mbeya wamehamasishwa kujitokeza kwa wingi katika mapokezi ya Spika wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini Dk ,Tulia Ackson Jumamosi Februali 26 mwaka huu ikiwa ni mara ya kwanza kufika jimboni kwake tangu achaguliwe katika nafasi hiyo
Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM Mbeya Mjini, Philipo Mng'ong'o amesema leo Alhamis Februari 24 ,2022 wakati wa chama kikitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusiana na ujio huo ,huku chama kikionya tofauti za kisiasa kuwekwa pembeni.
''Tunampokea Spika wetu wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini, Dk Tulia Ackson Jumamosi Februali 26 mwaka huu katika kata ya Nsalaga jijini hapa na baada ya hapo kutakuwa na mkutano wa hadhara katika viwanja vya Ruanda Nzovwe''amesema.
Amesema kuwa chama kina kila sababu ya kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kupendekeza jina la mgombea pekee wa nafasi ya Spika na wabunge kumpigia kura za kishindo jambo ambalo limeleta maono kwa wanambeya katika kupiga hatua za maendeleo.'' amesema.
Mstahiki Meya wa Jiji la Mbeya, Dourmohamed Issa amesema kuwa ni wakati sasa wa tofauti za kisiasa kuwekwa pembeni kwa kuwa na lengo moja la Mbeya kuwa ya kitofauti katika kuleta maendeleo kutokana na kupata Mbunge na Spika wa Bunge kwa mara ya kwanza tangu nchi ipate Uhuru.
'Sasa Mbeya tunaenda kuwa ya kitofauti kwa kupiga hatua za kimaendeleo hivyo ni wakati sasa Wananchi, viongozi kuunga mkono ujio wake na kujitokeza kwa wingi katika Mapokezi kwani tuna mifano hai ambayo tayari ameyafanya ''amesema.
Hata hivyo wakazi Jijini Mbeya wamesema watajitokeza kwa wingi kwenye mapokezi kwani ameleta heshima kwa Mkoa wa Mbeya na kutangaza kitaifa na kimataifa kwa kuwa na Spika wa bunge Mwanamke
Mkazi wa Ilomba Stephano Joseph amesema kuwa wana mbeya wanajivunia kupata Spika wa Bunge na Mbunge Mwanamke na Mbunge na kwamba ni wakati wao wa kumtumia katika kuleta maendeleo.
0 Comments