Rais wa Kenya William Ruto anakutana na marais wenzake wa Uganda Yoweri Museveni na Samia Suluhu wa Tanzania visiwani Zanzibar kujadili masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mawasiliano kutoka Ikulu nchini Tanzania imesema kuwa marais katika kikao hicho walikubaliana kuharakisha zoezi la ushirikishwaji wa wananchi kuhusu muundo na maeneo yatakayozingatiwa katika Rasimu ya Katiba ya Shirikisho la Kisiasa la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Zoezi hilo tayari limefanyika katika baadhi ya nchi za Afrika Mashariki zikiwemo Kenya, Burundi na Uganda.

Inatekelezwa na timu ya wataalam inayojumuisha wajumbe watatu kutoka kila Nchi Mwanachama.

Shirikisho la Kisiasa, kulingana na Museveni, litahakikisha ustawi wa watu kupitia soko kubwa huku pia likihakikisha usalama wao wa kimkakati.

Mkutano kati ya marais hao unaenda sambamba na mkutano wa Machi 14, 1996 wa Marais Daniel Arap Moi, Yoweri Museveni na Benjamin Mkapa ambao, uliweka msingi wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Shirikisho la Kisiasa litakapoundwa litajengwa katika mihimili mitatu; sera za pamoja za mambo ya nje na usalama, utawala bora na utekelezaji madhubuti.