NAIBU katibu Mkuu Wizara ya katiba na Sheria, DK Khatibu Katibu Kazungu amewataka watumishi wa ofisi za waendesha mashtaka nchini kuhakikisha wanatoa haki kwa kuzingatia taratibu, muongozo na wajibu.

DK Kazungu amesema hayo leo Machi 15, 2024  katika hafla ya ufunguzi wa jengo jipya la ofisi ya taifa ya mashtaka mkoani Shinyanga huku akieleza jengo hilo limegharimu zaidi ya Sh bilioni 2.1.

DK Kazungu amesema ufunguzi wa ofisi hiyo imejumlisha pia ufunguzi wa majengo mapya ya ofisi za waendesha mashtaka yaliyojengwa kwenye mikoa ya Pwani, Ruvuma, Manyara na Katavi.

“Tunampongeza Rais wetu wa Jamhuri wa muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassani kwa kutilia mkazo wa haki jinai na kuleta mageuzi makubwa katika haki jinai ni muhimu wananchi wakalata haki kwa wakati”amesema DK Kazungu.

DK Kazungu amesema mwaka huu kumekuwa na miradi 13 ya ujenzi wa ofisi ambapo mradi mmoja ni ujenzi wa ofisi moja iliyopo makao makuu, miradi sita ni majengo mapya ambayo yamekamilika na majengo sita mengine yapo kwenye hatua ya ukamilishaji

Akizungumza kwa kuwakilisha Kamati ya Kudumu ya Bunge, Utawala, Katiba na Sheria Boniface Botondo alisema kamati hiyo imesimamia vyema kuhakikisha bajeti inapatikana kuweza kupunguza changamoto zinazowakabili ikiwemo upatikanaji wa ofisi.

Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka nchini (DPP) Slyvester Mwakitalu kwa mwaka wa fedha huu wanatarajia kujenga majengo ya ofisi kwenye mikoa mitatu ikiwa Kuna wilaya 92 zinaofisi tayari huku wilaya 62 zimeanzisha ofisi.

“Changamoto iliyopo baadhi ya ofisi za wilaya na mikoa wamepanga na ofisi no finyu hali ambayo inaonyesha kukosekana kwa Uhuru wa mtu kutoa maelezo yake na uwazi,na waliopanga kwenye majengo ya halmashauri panapotokea kesi hukosa Usimamizi mzuri wa kutoa haki,” amesema.