Serikali inaweza kuanza tena kukata asilimia 1.5 ya ushuru wa Nyumba Nafuu kuanzia mwisho wa mwezi huu.

Haya yanajiri huku Rais William Ruto akisema kuwa Jumatatu atatia saini kuwa sheria Mswada wa Nyumba za Gharama Nafuu uliorekebishwa, 2023, unaozingatia sababu ambazo mahakama ilitaja ilipotangaza kuwa ni kinyume na katiba.

Ruto alikuwa akizungumza katika eneo bunge la Chepalungu, Kaunti ya Bomet, ambapo aliandamana na viongozi kadhaa akiwemo naibu wake Rigathi Gachagua, Waziri wa Barabara Kipchumba Murkomen na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah.

“Jumatatu naenda kuweka sahihi sheria mpya ya Affordable Housing ndio tuhakikishe ya kwamba tumeweka msingi dhabiti...tuhakikishe ya kwamba by next year tuwe na vijana elfu mia tatu ambao watakuwa wanafanya kazi kwa program ya Affordable Housing,” alisema.

Mahakama Kuu mnamo Novemba 28, 2023 ilitangaza ushuru wa nyumba kuwa kinyume na katiba, na kuamua kuwa ulikiuka Kifungu cha 10, 2 (a) cha Katiba.