KILIMANJARO: Jeshi la Polisi Nchini, limesema linatalajia kuwa, mwenyeji wa tukio la mafunzo ya utayari kwa vitendo (Field Training Exercise – FTX) mwaka 2024 litakalojumuisha nchi 14 wanachama wa Shirikisho la Wakuu wa Polisi Ukanda wa Mashariki  mwa Afrika (EAPCCO) kuanzia Aprili 13 – 18, 2024.

Akitoa taarifa hiyo leo Aprili 11,2024 Msemaji wa Jesh la Polisi Nchini naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime amesema tukio hilo la pamoja linatarajiwa kufanyika katika Shule ya Polisi Tanzania – Moshi ambapo takribani Maofisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wapatao 670 wanatarajiwa kushiriki.

DCP Misime amebainisha kuwa kufanyika kwa mazoezi hayo kunatokana na maazimio yaliyofikiwa na Wakuu wa Shirikisho la Polisi Ukanda wa Mashariki mwa Afrika katika mikutano yao ya kila mwaka.

Ameongeza kuwa katika mkutano uliofanyika mwezi Oktoba, 2021 Kinshasa nchini Kongo, wakuu hao wa polisi walipitisha azimio la zoezi hili kufanyika hapa nchini.

Pia amezitaja Nchi zinazotarajiwa kushiriki ni pamoja na mwenyeji Tanzania, Burundi, Eritrea, Djibouti, DRC Kongo, Kenya, Comoro, Ethiopia, Shelisheli, Rwanda, Somalia, Sudan, Sudani Kusini na Uganda.

Msemaji wa Jeshi hilo amebainisha kuwa lengo la shughuli hiyo na mazoezi mengine yaliyopita ni kuwajengea Maofisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali uwezo wa kubaini, kuzuia na kutanzua uhalifu unaovuka mipaka kama vile ugaidi, usafirishaji haramu wa binadamu, biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na kubadilishana uzoefu na taarifa za kitelejensia