Na Mwandishi wetu
SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imeunga mkono uanzishwaji wa Jukwaa la Tanzanite Ceo Roundtable Zanzibar Chapter na kuona ni moja ya njia itakayoweza kukuza na kuendeleza uwekezaji na biashara kwa kukuza uchumi wa nchi.

Pia imewataka Watendaji wakuu wa Sekta binafsi kutoka ndani na nje ya nchi kutumia Jukwaa hilo katika kuonyesha Serikali njia bora za kuzitumia kwaajili ya kuvutia uwekezaji zaidi Zanzibar.

Ameyasema hayo jana Visiwani Zanzibar,Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale,Mudrik Ramadhan Soranga katika uzinduzi rasmi wa Jukwaa hilo ambalo lilifuatiwa na meza ya majadiliano kuhusu Uwekezaji wa Biashara za ndani na Kujenga Uchumi wa Bluu Imara Zanzibar.

Soranga amesema uzinduliwaji wa Jukwaa hilo kwa zanzibar ni moja ya mkakati wa kuzidi kuongeza uaminifu zaidi kwa wawekezaji na kuonekana ni sehemu sahihi na salama kwa kufanya uwekezaji na biashara.

''Kwa upande wa Zanzibar tumefurahi sana,kuzinduliwa kwa Chapter hii kwa sababu kuwepo kwa Jukwaa hili ambalo limewakutanisha watendaji wakuu wa Kampuni mbalimbali binafsi ni muhimu sana kwa nchi,hata wawekezaji wengine wanapotaka kuja kuwekeza Zanzibar,mara nyingi uwa wanauliza kama kuna Jukwaa kama hili ambalo wanaweza kukutana nao na kuwapa uzoefu juu ya uwekezaji na ufanyaji wa biashara kwa Zanzibar,''amesema na kuongeza

''Katika miaka hii minne ya serikali ya awamu ya nane kumekuwa na muamko mkubwa sana wa uwekezaji Zanzibar hususan katika sekta ya utalii lakini bado tunataka kufungua wigo mpana zaidi katika kufungua sekta nyingine nyingi ambazo wawekezaji wakija wanaweza kuzifanya ikiwemo katika masuala ya ICT ambalo ni eneo la kimkakati ukiangalia uchumi wa visiwa na mazingira mazuri ambayo yanaweza kufanya masuala ya tehama,''amesema.

Kwa Upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi,Uchumi na Uwekezaji Zanzibar,Shariff Ali Shariff amesema uwepo wa kuanzishwa kwa Jukwaa hilo kwa Zanzibar ni jambo zuri na muhimu katika kukuza uchumi wa nchi.

Amesema Serikali imejipanga kuhakikisha inashirikiana na Watendaji hao wakuu wa Makampuni binafsi katika kuwapa ushirikiano na msaada unaohitajika ili kuhakikisha matajiri wanaoongezeka Zanzibar na kuwa na mchango mkubwa kwa kukuza uchumi.

''Nchi hii kupitia Sekta binafsi inakuwa na kukua kwake kunategemea uwepo wa makampuni binafsi ambao wanaungana katika kuzungumza na kuona namna gani wanaweza kutengeneza mitaji na kukuza biashara zao,''amesema.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Tanzanite CEO Roundtable Chapter ya Zanzibar,Dkt.Josephine Kimaro amesema Jukwaa hilo linawakutanisha Maafisa watendaji wakuu hasa kutoka katika sekta binafsi kwa lengo la kujifunza wao kwa wao,kutengeneza mtandao kati yao na kuweza kuhakikisha wanapeana sapoti inayotakiwa ili kuweza kukuza sekta binafsi na biashara zao.

''Katika utendaji kuna changamoto mbalimbali hivyo wanapokutana katika majukwaa kama haya na kuzungumza wanaweza kupeana ushauri na kusaidiana kutatua changamoto ambazo zinazowakabili,''amesema na kuongeza

''Jukwaa hili limekuja wakati muafaka ambapo uchumi wa Zanzibar unakua na uwekezaji mkubwa unaoendelea kutokea pamoja na fursa mbalimbali ambazo sekta binafsi wanauwezo wa kuchukua na kuzifanyia kazi kuleta matokeo chanya,''amesema.

Akitaja miongoni mwa vitu ambavyo wanaweza kujadiliana watendaji wakuu hao wanapokutana ni pamoja na kukuza brand zao,mitaji yao na kutatua masuala mbalimbali yanayohusiana na ajira katika upande wa sheria na taratibu mbalimbali.

Aidha Mwenyekiti wa Ceo Roundtabe Chapter ya Kenya,Suzan Ng'ong'a amesema kupitia jukwaa hilo linawapa fursa watendaji hao kukaa pamoja na kushirikiana kujenga biashara kukuza uchumi wao pamoja na uongozi .

Amesema majukwaa haya yanafaida kubwa kwao kama watendaji wakuu katika kuona viwango vya maaadili katika kazi zao na kampuni zao katika kukuza uchumi.