Serikali ya Benin imetangaza kuwa imefanikiwa kuzima jaribio la mapinduzi lililofanywa na baadhi ya wanajeshi wa taifa hilo la Afrika Magharibi.

“Jeshi la Benin na viongozi wake, wakiwa waaminifu kwa kiapo chao, wamesalia kuwa waaminifu kwa jamhuri,” alisema Waziri wa Mambo ya Ndani, Alassane Seidou, katika hotuba iliyotangazwa kwenye televisheni.

Mapema Jumapili, kundi la wanajeshi lilitoa matangazo kwenye runinga yakidai kwamba yamepindua na kumvua madaraka Rais Patrice Talon. Mashuhuda waliiambia BBC kwamba walisikia milio ya risasi na baadhi ya wanahabari wa televisheni ya taifa kushikiliwa mateka.

Mshauri wa rais ameieleza BBC kuwa kiongozi huyo yuko salama na yuko katika ubalozi wa Ufaransa. “Asubuhi ya Jumapili, tarehe 7 Desemba 2025, kundi dogo la wanajeshi lilianzisha uasi uliolenga kuyumbisha nchi na taasisi zake,” Seidou alisema.

Hata hivyo, wanajeshi watiifu serikalini waliweza “kurejesha udhibiti wa hali hiyo na kuzuia jaribio hilo,” aliongeza.

Helikopta zimeonekana zikizunguka juu ya mji mkuu wa Cotonou makao ya serikali na barabara zimefungwa huku kukiwa na ulinzi mzito wa jeshi katika mitaa kadhaa.

Benin, koloni la zamani la Ufaransa, kwa muda mrefu imejulikana kama moja yanchi zenye demokrasia thabiti barani Afrika.

Ni moja ya nchi wazalishaji wakubwa wa pamba barani, ingawa inasalia miongoni mwa nchi masikini zaidi duniani