DODOMA; Serikali imesema kanuni ya kikokotoo kwa wastaafu hutumika kwa wafanyakazi wote walioajiriwa sekta ya umma na binafsi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu ametoa kauli hiyo bungeni leo Agosti 31, 2026 alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Baraza la Wawakilishi, Said Ali Mbarouk aliyehoji serikali ina mpango gani kuondoa utaratibu wa sasa wa kikokotoo kwa wastaafu wa Jeshi la Polisi ili kuboresha maslahi kwa wastaafu.

“Dhamira ya Serikali ni kuendelea kuboresha mafao ya wastaafu wote ikiwemo wa Jeshi la Polisi kadri mifuko ya pensheni inavyoimarika na si kuondoa utaratibu uliopo sasa unaotumika kulipa mafao.

“Mifuko ya pensheni inatumia Kanuni Maalumu au Kikokotoo katika kulipa mafao kwa wanachama wanaochangia katika Mifuko hiyo.

Kanuni hii hutumika kwa wafanyakazi wote walioajiriwa katika sekta ya umma na binafsi ikiwemo Jeshi la Polisi.

“Aidha, kanuni hairuhusu kuwa na ukokotoaji tofauti katika Mfuko wa Pensheni kwa wanachama wenye sifa zinazofanana,” amesema.