RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa kuwezesha Idara ya Uhamiaji kuendelea kuboresha na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa huduma za Uhamiaji, hatua inayolenga kurahisisha na kuongeza ufanisi katika taratibu za kuingia na kutoka nchini kwa raia na wageni.
Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Patrobas Katambi na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji CGI Dkt. Anna Makakala wakati wa uzinduzi wa darasa la mafunzo ya mfumo huo katika Chuo Cha Uhamiaji Cha Kikanda TRITA Moshi Mkoani Kilimanjaro Septemba 2026.
Katika hatua hiyo ya mageuzi ya kidigitali, Idara ya Uhamiaji inatarajia kuanza kutumia mifumo mipya ya kiteknolojia katika vituo vya kuingia na kutoka nchini, ikiwemo Mfumo wa Advanced Passenger Information System (APIS) na Passenger Name Record (PNR).
Pia mifumo hiyo itawezesha upatikanaji na uchakataji wa taarifa za abiria kwa njia ya kidigitali kabla na wakati wa safari, jambo litakalosaidia maofisa uhamiaji kupata taarifa muhimu kwa wakati na hivyo kuwezesha huduma za uingiaji na utokaji nchini kutolewa kwa uharaka na ufanisi zaidi.
Aidha hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuwekeza katika teknolojia na mifumo ya kisasa inayolenga kuboresha huduma kwa wananchi na wageni, huku ikiimarisha taratibu za usimamizi wa mipaka na usalama wa Taifa.
Kupitia maboresho hayo, Idara ya Uhamiaji Tanzania inaendelea kujikita katika matumizi ya teknolojia ya kidigitali ili kutoa huduma bora, salama, zenye ufanisi na zinazokwenda sambamba na viwango vya kimataifa.
Mifumo hiyo mipya inatarajiwa kuanza kufanya kazi hivi karibuni katika vituo husika vya kuingia na kutoka nchini.

0 Comments