KUTOKANA na utafiti wa kisayansi kuonesha kuwa kutofanya tohara kwa wanaume ni moja ya sababu zinazochangia maambukizi ya Ukimwi, wanaume katika mikoa saba nchini wanatarajiwa kufanyiwa tohara kuanzia mwakani kwa sababu inayo idadi kubwa ya wanaume wasiotahiriwa.

Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imesema itaanza operesheni maalumu kwa kushirikiana na wadau wengine yakiwemo mashirika ya misaada kutoka Marekani, kufanya tohara kwa wanaume hao katika mikoa ya Mbeya, Iringa, Rukwa, Kagera, Tabora, Shinyanga na Wilaya ya Rorya mkoani Mara.

Hayo yalibainishwa na Waziri wa Wizara hiyo, Dk. Haji Mponda, jana mjini hapa, katika hotuba yake kabla ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kumkaribisha Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal kuhitimisha maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani, Kitaifa mjini hapa.