MFUMO wa ulipaji nauli kwa mabasi ya abiria jijini Dar es Salaam na miji mingine nchini maarufu kama daladala, express na vifodi, uko mbioni kubadilika kwa abiria kulazimika kulipa nauli kwa kilometa watakazosafiri.

Hayo yamo katika mapendekezo ya Chama cha Wamiliki wa Daladala Dar es Salaam (DARCOBOA), kinachopendekeza ongezeko la nauli, lakini katika mfumo wa kulipa kwa kilometa.

Imependekezwa, mtumiaji wa daladala alazimike kulipia Sh 51 kwa kilometa, ili wamiliki wa vyombo hivyo vya usafiri wamudu gharama za uendeshaji ambazo zimekuwa zikiongezeka siku hadi siku.

Hii ina maana kwamba, endapo pendekezo hilo litapita, kwa abiria anayetoka kwa mfano Bunju kwenda katikati ya Jiji, atalazimika kulipa Sh 1,530 kwa safari moja, na kama atarudi, basi kwa siku atalipa Sh 3,060.