Serikali ya Japan imesema, mionzi kutoka kwenye mtambo wa nyuklia wa Fukushima Daiichi uliokumbwa na tetemeko kubwa la ardhi umefikia kiwango cha kuleta madhara.
Onyo hilo lilitolewa baada ya mtambo huo kutikiswa na mlipuko wa tatu, unaoonekana kuharibu mfumo wa kuhifadhi kinu kimojawapo kwa mara ya kwanza.
Iwapo itakuwa imepata ufa, kuna wasiwasi wa kuvuja kwa mionzi zaidi.
Maafisa wameongeza umbali wa eneo la hatari, wakionya wakazi walio ndani ya kilomita 30 kuondoka au kubaki ndani ya nyumba zao.
Baadae serikali ilisema viwango vya mionzi katika lango kuu la mtambo huo vimeshuka.

Mtikisiko huo umechochewa na tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 9.0 lililotokea Ijumaa iliyopita na tsunami kaskazini-mashariki mwa Japan.
Siku ya Jumanne, kinu nambari 2 kilikuwa cha tatu kulipuka katika kipindi cha siku nne kwenye mtambo huo wa Fukushima Daiichi.
Moto nao ulizuka ghafla katika kinu nambari 4, na kuaminiwa kusababisha kuvuja kwa mionzi.
Kinu nambari 4 kilifungwa hata kabla ya tetemeko hilo kwa ajili ya matengenezo, lakini vyuma vya kinyuklia vya mafuta vilivyotumika bado vimehifadhiwa kwenye eneo hilo.
Katibu wa baraza la mawaziri Yukio Edano alikuwa akingalia kwa makini vinu viwili viliyobaki kwenye mtambo nambari tano na sita, kwani vilianza kupata joto kiasi.
Alisema maji ya bahari ya kupooza yamekuwa yakitiwa kwenye kinu nambari moja na tatu- ambavyo vimekuwa vikirudi katika hali yake ya kawaida- na pia kwenye kinu nambari 2, ambacho hakitabiriki.
Kiwango cha mionzi kwenye mji mkuu wa Japan- umbali wa kilomita 250- kimeripotiwa kuongezeka kuliko kawaida, lakini maafisa wamesema hakuna hatari zozote za kiafya zinazoweza kutokea.
Wakazi wa Tokyo wamekuwa wakikusanya vifaa, huku maduka mengine yakiishiwa na bidhaa kama vile chakula, maji, barakoa na mishumaa.