MVUA kubwa iliyonyesha katika milima ya Mbulu na Karatu, imesababisha mafuriko yaliyosomba majabali ya mawe na kufunga barabara kuu ya Karatu - Arusha.

Hali hiyo imesababisha watalii wa mbuga za wanyama za Manyara, Ngorongoro na Serengeti na huduma za usafiri wa mabasi katika wilaya za Karatu na mkoani Mara kukwama kuanzia juzi usiku.

Mbali na kuathiri shughuli za usafirishaji, pia familia zaidi ya 25,000 katika mji wa Mto wa Mbu
wilayani Monduli kwa sasa hazina mahali pa kuishi kutokana na mvua hiyo iliyoendelea usiku wa kuamkia jana na kusababisha maafa ndani ya nyumba zaidi ya 25,000 za mji huo. 
 
Majabali hayo yalisombwa na maji ya Mto Kirurumo ulioanzisha mkondo mwingine wa maji na kuyarundika katika barabara ya Arusha-Karatu na kusababisha msongamano mkubwa wa magari.

Mamia ya magari ya utalii, magari binafsi na ya abiria madogo kwa makubwa yalikwama
barabarani na kusababisha adha kubwa Mto wa Mbu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya kutembelea eneo la maafa, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, alikiri kuwa hali ni mbaya na inapaswa kusimamiwa kikamilifu ili huduma za usafiri zirejee kama zamani, vinginevyo pato la Taifa litapungua.

Mulongo alisema mlinzi wa Hoteli ya Serena, Ndaheto Kurudimu (35), alipoteza maisha baada
ya kusombwa na maji na majabali umbali wa zaidi ya kilometa tano.

Mulongo alisema uongozi wa Mkoa ukishirikiana na wakuu wa wilaya za Karatu na Monduli, utahakikisha huduma za usafiri zinarejea ndani ya saa 48.

Alisema Novemba 18 eneo la Makuyuni, kulitokea mafuriko yaliyoua watu wawili ambao
hakuwa na majina yao na kueleza kuwa hadi jana watu watatu walikuwa wamekufa katika maafa
mengine yaliyotokea Monduli.



Mulongo alisema uongozi wa Mkoa kwa kushirikiana na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) na taasisi nyingine, wanashirikiana kuleta matingatinga ya kuondoa mawe yaliyosombwa barabarani ndani ya
muda huo, ili huduma za kiuchumi ziendelee kama kawaida.

‘’Hali ni mbaya, majabali makubwa ya mawe yamesombwa na yako barabarani na makalavati
zaidi ya sita yamesombwa. Kwa sasa huduma ya usafiri ni mbaya sana lakini tunajitahidi kupambana na hali hiyo,’’ alisema Mulongo.

Alisema Serikali imejipanga kuhakikisha familia zote zilizopata athari ya nyumba zao kuingiwa na maji, zinapata huduma ya chakula na dawa na kuahidi kuwa hakuna mtu atakayekufa na njaa.

‘’Sasa hivi tunafanya tathmini ya kujua hatua gani zichukuliwe kwa haraka, ili wananchi wote
waliopatwa na janga wapate huduma za chakula na dawa,’’ alisema.

Diwani wa Kata ya Mto wa Mbu, Abeli Abeli, alisema mvua iliyonyesha katika mji huo haijapata kutokea kwa zaidi ya miaka 20 na janga hilo linapaswa kushughulikiwa ipasavyo ili huduma za utalii na abiria zirejee.

Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, alifika eneo hilo na kujionea jinsi wapiga kura wake
walivyoathirika na hali hiyo.

‘’Nimefika katika eneo la tukio lakini nataka kujua hali halisi ya athari iliyowapata wapiga kura
wangu ili nijue cha kuwasaidia,’’ alisema Lowassa.