STAA wa filamu, Flora Festo Mvungi, anateswa na mapenzi, hivi sasa anajuta kumpa penzi lake mwanamuziki Hamis Ramadhan Baba ‘H.Baba’.

Flora, alikisanua mbele ya mwandishi wetu wiki iliyopita kwamba kinachomfanya ajute kuwa na H. Baba ni namna ‘brazameni’ huyo anavyombana.

“Nabanwa sana na huyu mwanaume, yaani kila kona anataka niwe naye, sasa tunakuwa hatuwezi kufanya kazi za kimaendeleo, kila nikipokea simu, anataka ajue ni nani,” alisema Flora akifuta machozi na kuongeza:
“Hamis (H. Baba) ana wivu sana, ndiyo maana najuta kuwa naye.”

Msanii huyo ambaye alikutwa na paparazi wetu akiwa amejiinamia, huku akitokwa na machozi, Kinondoni, alisema kuwa hivi sasa anakosa ‘dili’ nyingi za kucheza filamu kwa sababu ya kubanwa na H. Baba.

“Kwa kweli inabidi niwe makini. Nisipokuwa mwangalifu nitazidi kufulia kwa huyu mwanaume. Nilichokuwa nakitarajia katika mapenzi kutoka kwake sicho ninachopata,” alisema.


Kutokana na hali hiyo, Flora alisema kuwa uamuzi wake kwa sasa ni kutafuta watu wenye busara wazungumze na H. Baba ili abadilike na kama asipoona mabadiliko, ataamua waachane.

Kutokana na malalamiko hayo, paparazi wetu ‘alimvutia waya’ H. Baba ambaye alisema:
“Katika uhusiano wa kimapenzi au ndoa, kugombana ni suala la kawaida. Kumfuata Flora kila aendapo ni halali yangu maana ni mchumba wangu isipokuwa watu wanajaribu kuingiza maneno ili tutengane,” alisema H. Baba na kuongeza:

“Kama Flora alisema hayo basi zilikuwa ni hasira, maana kutofautiana kulitokea zamani na sasa tunaelewana vizuri. Haiwezi kutokea tena na wanaosubiri tuachane, basi watasubiri sana. Kama kuna makosa ya kibinadamu basi tutayamaliza,” alisema H. Baba kwa kisingizio kuwa yupo uwanjani hivyo hawezi kuongea kwa upana juu ya suala hilo.