Takriban wapiganaji 35 wa kundi la kiisilamu la Boko Haram, wameuawa katika msako mkali dhidi ya kundi hilo Kaskazini Mashariki mwa Nigeria.
Kwa mujibu wa jeshi la Nigeria, wapiganaji wengine sitini walikamatwa wakati wa msako huo kwenye majimbo ya Adamawa na Yobe.
Kundi hilo la kiisilamu, linapinga mifumo ya kimagharibi na athari zake nchini Nigeria na wamekuwa wakifanya mashambulizi yanayolenga maslahi ya nchi za Magharibi pamoja na makanisa.

Mnamo siku ya Jumapili, kulitokea shambulizi dhidi ya kanisa moja katoliki na ambalo lilisababisha mauaji ya watu wawili. Boko Haram ndilo limelaumiwa kwa kufanya shambulizi hilo.

Msemaji wa jeshi nchini humo, alifahamisha shirika la habari la AFP kuwa msako huo ulifanyika usiku kucha kati ya siku ya Jumapili na Jumatatu.

Wanajeshi walifanya msako wa nyumba hadi nyumba, katika mitaa mitatu na wakati mwingine kufyatuliana risasi na wapiganaji hao, usiku kucha.

Wanajeshi wawili walijeruhiwa katika makabiliano hayo.

Bunduki na mabomu vilipatikana katika maficho ya wanamgambo hao pamoja na silaha zengine ikiwemo mishale 32 na panga.

Mji huo umekuwa mojawapo ya miji iliyoathirika sana kutokana na harakati za Boko Harama ambalo linataka kutumika kwa sheria za kiisilamu kote nchini humo.