Shuhuda wa ajali hiyo, Paulina Ruge (57) ambaye ni mmiliki wa nyumba iliyogongwa na basi hilo, alisema ilitokea kati ya saa 4:30 na 5:00 asubuhi.PICHA|MAKTABA

Busega. Watu 10 wamekufa papo hapo na mwingine kupoteza maisha alipokuwa akipelekwa hospitali baada ya basi walilokuwa wakisafiria kupata ajali mkoani Simiyu. Ajali hiyo ilitokea eneo la Itwilima A, Kata ya Kilorei, Wilaya ya Busega baada ya basi hilo la Luheye lifanyalo safari zake kati ya Bunda na Mwanza kupata hitilafu na kugonga mti na baadaye nyumba. Akizungumza katika Hospitali ya Wilaya ya Magu jana, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Pascal Mabiti alisema watu waliokufa ni 11 na majeruhi 44. Mabiti alisema mtu mmoja aliyefariki wakati akipelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando jina lake bado lina utata... “Jina la huyu mama ambaye ameacha watoto watatu; Joyce Wilson (6), Jenipher Wilson (3) na Jack (miezi miwili), wametwambia mama yao alikuwa anaitwa Lucia Wilson, lakini taarifa tulizopata kutoka Bugando zinasema alikuwa anaitwa Fodia Guniniga.”Alisema majeruhi 19 ni wanawake na 25 wanaume na kwamba, wachache wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Magu lakini wengi walipelekwa Bugando kutokana na hali zao kuwa mbaya. “Natoa wito kwa wananchi kwenda Hospitali ya Bugando Mwanza kutambua maiti. Miili ya watu wote waliokufa tumeihifadhi hapo na hakuna aliyetambuliwa zaidi ya huyo mama ambaye ameacha watoto watatu,” alisema.

Shuhuda wa ajali hiyo, Paulina Ruge (57) ambaye ni mmiliki wa nyumba iliyogongwa na basi hilo, alisema ilitokea kati ya saa 4:30 na 5:00 asubuhi. Alisema baada ya ajali alishuhudia ikitolewa miili ya watu 10 waliokufa. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, Charles Mkumbo alisema baada ya kutokea ajali hiyo dereva ambaye jina lake halijafahamika alikimbia na polisi wanaendelea kumtafuta.