Katika hukumu nadra kutolewa nchini Tanzania, mahakama Kuu Kanda ya Tabora imeiagiza halmashauri ya wilaya ya Urambo, kulipa fidia ya shilingi milioni 25 kwa Mwamini Adam na mumewe Idrisa Jafari kutokana na madhara waliyopata baada ya uzembe uliofanywa na daktari wa hospitali ya wilaya hiyo alipokuwa akimfanyia upasuaji Mwamini.
Katika uamuzi wa shauri hilo la madai Namba 13/2011 uliotolewa hivi karibuni, Mahakama Kuu imeiagiza halmashauri hiyo kumlipa Mwamini shilingi milioni 20 kutokana na kilema alichopata kwa kuondolewa mfuko wa uzazi na kukatwa utumbo. Pia, mahakama imeiagiza halmashauri hiyo kumlipa Jafari fidia ya shilingi milioni tano ikiwa ni gharama za uendeshaji wa shauri hilo.
Akisoma hukumu, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Amir Mruma alikubaliana na madai ya walalamikaji kuwa madhara waliyopata kutokana na uzembe uliofanywa na Dk Jackob Kamanda ni makubwa.
Jaji Mruma alisema haipingiki kwamba huo ni uzembe uliofanywa na mtumishi, hivyo mwajiri anapaswa kulipa gharama.
Aliagiza kuwa kiwango hicho cha fedha kitalipiwa riba ya asilimia saba kila siku kuanzia tarehe ya uamuzi ulipotolewa hadi siku mlalamikiwa atakapolipa fedha hizo.
Mwamini na mumewe walifikisha malalamiko yao Mahakama Kuu, wakidai kulipwa fidia ya shilingi milioni 505 kutokana na makosa ya uzembe uliofanywa na wataalamu wakati wa upasuaji kwa kuacha kitambaa tumboni mwa mgonjwa.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake, Anatory Lukonge wa Hospitali ya Itigi ambako walibaini kitambaa tumboni mwa Mwamini, aliieleza mahakama kuwa walipomfanyia upasuaji walikuta utumbo umeshikana na kizazi huku juu yake kukiwa na kitambaa.
Dk Lukonge alisema walikitoa kitambaa hicho lakini kutokana na sehemu ya kizazi kuharibika, iliwalazimu kukiondoa huku akidai kuwa hali hiyo ilisababishwa na uzembe wa daktari aliyemfanyia upasuaji.