Sifael Paul
Hatari! Masistaduu wawili kunako gemu la Bongo Movies, Wema Isaac Sepetu na Jacqueline Wolper Massawe, wamejikuta wakipiga ulabu hadi kulewa chakari, kisa kikielezwa kwamba wana msongo wa mawazo, Risasi Jumamosi linafunguka.
Masistaduu wawili kunako gemu la Bongo Movies, Wema Isaac Sepetu na Jacqueline Wolper Massawe wakipiga mtungi usiku mnene.
ENEO LA TUKIO KINONDONI-MANYANYA
Tukio hilo lililoshuhudiwa na gazeti hili lilijiri hivi karibuni, usiku mnene kwenye pati ya kuzaliwa (birthday) ya meneja wa kampuni ya Wema ya Endless Fame almaarufu Petit Man iliyofanyika kwenye nyumba ya jamaa mmoja maeneo ya Kinondoni-Manyanya jijini Dar na kuhudhuriwa na mastaa kibao.
Katika pati hiyo ambayo mbali na mastaa ilihudhuriwa na watoto wa mjini, watu waligonga msosi wa kufa mtu kisha vikafuata vinywaji.

Tofauti na ‘maraia’ wengine, Wema na Wolper walikuwa wakigonga vinywaji vikali hadi wakawa tilalila na kuanza kufanya vituko, jambo ambalo liliwashangaza wengi.Kadiri muda ulivyokuwa unasonga ndivyo mastaa hao walivyozidi kucharuka tofauti na walipofika kwani walionekana wapole na wastaarabu kupita maelezo.
Baada ya ulabu kuwakolea walianza kupigana picha kwa simu kisha kukata mauno kabla ya Wolper kuzimika kufuatia kuzidiwa na ‘kinywaji’.Kwa upande wake Wema alimpiga vibao mwanaume shoga aliyetajwa kwa jina moja la Danny baada ya kutibuana kabla ya watu kuwaamulia.Ulipofika muda wa kuondoka mahali hapo, ilidaiwa kwamba Wolper ilibidi abebwe ili kupelekwa kwenye gari kwani alikuwa hajiwezi.
Wema Isaac Sepetu na Jacqueline Wolper wakifurahia jambo.
KISA MSONGO WA MAWAZO
Uchunguzi wa Risasi Jumamosi umebaini kwamba, mastaa hao wana msongo wa mawazo hivyo wanaona njia pekee ya kuwaondolea ‘stresi’ ni kunywa pombe.

WEMA
Habari za ndani zilieleza kwamba, tangu Wema ameachana na staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ amekuwa mtu mwenye mawazo na njia pekee ambayo huitumia ni kujipooza kwa pombe kali.
“Ndiyo maana ana mpaka kaunta ya pombe kali nyumbani kwake,” alisema mmoja wa watu wake wa karibu (Team Wema).

ZARI ATAJWA
Ilisemekana kwamba mbali na mawazo ya Diamond ambaye amehamia kwenye nyumba ambayo Wema alikuwa na mchango mkubwa wakati wa ujenzi, pia suala la jamaa huyo kutanua na mpenzi wake wa sasa, Zarinah Hassan ‘The Boss Lady’ limekuwa likimpa wakati mgumu mwanadada huyo.

Staa katika tasnia ya filamu, Bongo Wema Isaac Sepetu.
SUALA LA UGUMBA
Habari zilieleza kuwa, jambo lingine linalompa Wema msongo wa mawazo ni suala la kukosa mtoto kila anapomtafuta akiamini kuwa watu wanajua yeye ni mgumba.Pia ilielezwa kwamba kuna suala la kuishiwa na kuogopa kufilisika kwani kwa sasa filamu hazilipi na bado anataka kuendelea kuwa na heshima ya kuitwa Madam hivyo njia pekee anayoona inafaa kutuliza mawazo ni kunywa pombe.

WOLPER
Kwa upande wake Wolper uchunguzi ulionesha kwamba, kwanza anapenda fedha hivyo kukosa tenda za kuigiza na kuanguka kwa soko la filamu za Kibongo kumemsababishia msongo wa mawazo kama ilivyo kwa Wema kwani naye anataka kuishi maisha ya kistaa ambayo hayawezekani bila kuwa na mshiko.

WOLPER KALOGWA?
Akizungumzia hali hiyo, Wolper alikiri kuwa na mawazo mengi huku akihisi kuwa huenda amelogwa.
USHAURI WA KISAIKOLOJIA

Staa katika tasnia ya filamu, Bongo Jackline Wolper.
Kwa mujibu wa mtaalam wa saikolojia aliyezungumza na gazeti hili juu ya mastaa aliwashauri kama ifuatavyo;
Mtaalam huyo alishauri mastaa hao kuachana na pombe na kama wana mawazo ya kuumiza, wanatakiwa kujilazimisha kutabasamu mara kwa mara na kusahau jambo linalowaletea mawazo mabaya.

Alisema kuwa, kutabasamu kutawasaidia kuchangamsha akili, ingawa inaweza kuchukua muda kurudi katika hali ya kawaida lakini inasaidia kuamsha hisia za furaha zilizokuwa zimeshambuliwa na mawazo mabaya na kuamini katika ushindi.
WASISAHAU NYUMBA ZA IBADA
Pia aliwashauri kusahau mambo yaliyopita na kujikita katika kufanya kazi kwa bidii hata kama matunda hawayaoni sasa, yatakuja baadaye.Mbali na hivyo wajitahidi kujichanganya katika makundi ya watu sahihi na kujumuika kwenye nyumba za ibada, msikitini (kwa muislam) na kanisani (kwa mkristo).