RAIS Jakaya Kikwete amelihutubia Bunge la Kenya na kuwaaga wananchi wa Kenya huku akisisitiza ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya kwamba utadumu milele. Aidha, amesema anaamini Wakenya watakuwa wamepata fundisho kutokana na machafuko yaliyotokana na uchaguzi wa mwaka 2007 na hawatarudia tena.
Katika hotuba yake aliyotumia lugha ya Kiingereza kwa dakika 15 na kisha akaombwa kuzungumza kwa Kiswahili na wabunge na maseneta, Rais Kikwete alisema uhusiano wa Kenya na Tanzania ni wa kidugu zaidi na kwamba hata kama anaondoka madarakani, anaamini utaendelea kwa sababu zipo sababu za msingi za kufanya hivyo.

Alisisitiza kuwa, Kenya ni mshirika mkubwa wa Tanzania katika maendeleo na kwamba kwa vyovyote, vile sera hiyo haitabadilika kutokana na umuhimu wake. Akifafanua, alisema Kenya na Tanzania zimekuwa washirika wakubwa katika masuala ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na kidiplomasia, hali ambayo inaifanya iendelee kuwa na ushirikiano wa kudumu.
Akitoa mfano, alisema kumekuwa na ushirikiano katika kuunganisha barabara za nchi hizo, kwenye huduma za umeme, na sasa hivi mradi mpya wa gesi ya Mtwara ambayo Kenya itanunua kutoka Tanzania.
“Katika mazungumzo na Rais Uhuru Kenyatta tulikubaliana kuanza mradi wa kupeleka umeme Kenya na tutaanza na kilovoti 400 kwa kujenga mtambo wa kupeleka umeme huko,“ alisema Rais Kikwete.
Alisema kilovoti hizo 400 ni sehemu ya mahitaji ya kilovoti 1000 ambayo Kenya itapatiwa na Tanzania katika mradi huo. Pia alisema, kuhusiana na gesi Kenya itanunua gesi kutoka Tanzania ili kurahisisha maendeleo ya nchi hiyo kwa sababu itapatikana kwa bei rahisi na itakuwa ya kuaminika.
Kuhusu siasa aliwakumbusha kwamba ni vyema Kenya mpya ikaendelea kuwa ya amani na utulivu na kwamba machafuko ya 2007 yawe ni fundisho kwao. Aliwaahidi wabunge na maseneta wa Kenya kwamba atabaki kuwa rafiki wa kweli wa Kenya na kwamba baada ya kumaliza muda wake wa uongozi atakuwa anawatembelea mara kwa mara.
Apewa barabara ya Ikulu Aidha, wakati leo akiadhimisha miaka 65 ya kuzaliwa kwake, mapema jana Rais Jakaya Kikwete alipewa zawadi ya kudumu ya bethidei nchini hapa, baada ya Mamlaka ya Jiji la Nairobi kuipa jina lake moja ya barabara za jiji hilo.
Rais Kikwete ambaye jana alihitimisha ziara yake ya siku tatu ya kiserikali nchini Kenya, atakumbukwa daima hapa baada ya Barabara ya Mlimani sasa kuanzia jana itajulikana kwa jina la Barabara ya Jakaya Kikwete. Barabara hiyo inaanzia katika makazi ya Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, karibu kabisa na Ikulu ya nchi hii.
Rais Kikwete alizindua barabara iliyopewa jina lake jana saa tano asubuhi katika eneo jirani na geti la kuingia katika makazi ya Rais Uhuru. Katika shughuli hiyo, vijana wa eneo hilo la Jimbo la Dagoretti North ambalo Mbunge wake ni Simba Arat na anayeonekana kupendwa na wananchi wake, walikuwa wamebeba mabango yenye ujumbe wa kufurahia Rais Kikwete kupewa barabara hiyo, huku wakiimba na kucheza wimbo maarufu wa My Number One wa msanii Nassib Abdul `Diamond Platnumz’ wa Tanzania.
Mabango hayo mawili yalikuwa yameandikwa, “Vijana wa Mlimani sasa ni vijana wa Kikwete,” na jingine “Kikwete karibu Kikwete Road.” Akizungumza katika shughuli hiyo, Gavana wa Kaunti ya Nairobi, Evans Kidero alisema mara nyingi watu kwa Kenya vitu hupewa majina ya wapendwa wao.
Alisema moja, watu huwapa majina watoto wao kutokana na majina ya marafiki zao na kwa Kenya, jina la Rais Kikwete wamepewa watoto wengi. Gavana aliongeza kuwa na pia majina ya marafiki wapendwa hupewa shamba au barabara, ndio maana wameamua kuipa barabara hiyo jina la Rais Kikwete.
“Kutokana na urafiki wako mkubwa na uhusiano mwema na Rais Uhuru Kenyatta, barabara hii ya Mlimani Road, sasa itajulikana kwa jina la Barabara ya Jakaya Kikwete,” alisema Kidero na kuongeza: Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Kikwete alisema hana maneno ya kutosha kuonesha furaha yake kwa uamuzi huo wa Jiji la Nairobi kumpa barabara yenye jina lake.
“Rais Uhuru jana (juzi) aliniuliza kuhusu suala hilo kama nalikubali, nami nilimjibu kama mmeamua hivyo, sina pingamizi. Mmenikabidhi funguo za Jiji la Nairobi na sasa mmeipa barabara jina langu, hii ni habari kubwa. Rais Kikwete pia jana alitembelea kiwanda cha magari cha General Motors East African Limited, na baadaye kulihutubia Bunge la Kenya na jioni alirejea nchini.