JESHI la Polisi nchini limekemea tabia inayoendelea kujengeka miongoni mwa baadhi ya wananchi ya kutoheshimu sheria na kujichukulia sheria mikononi kwa kuwapiga, kuwadhalilisha watuhumiwa, kuwachoma na kuwaua.
Aidha imetangaza zawadi kwa mwananchi yeyote atakayerekodi tukio la aina hiyo na kulifikisha kwao. Imeelezwa kuwa kuanzia Januari hadi Oktoba mwaka huu, watuhumiwa 829 wameuawa na wananchi.

Polisi imewaomba wananchi kutoa ushirikiano wa kutosha kukomesha tabia hiyo na kuahidi kuwa mwananchi yeyote atakayerekodi tukio la watu wanaojichukulia sheria mkononi na kulifikisha polisi kwa siri atapewa zawadi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Msemaji wa jeshi hilo, Advera Bulimba alisema idadi ya watu hao waliokufa imeongezeka ikilinganishwa na watuhumiwa 785 waliouawa kwa sababu kama hizo kwa kipindi kama hicho mwaka 2014.
“Katika siku za hivi karibuni, kumeibuka tabia hiyo ya wananchi kujichukulia sheria mkononi na kuwafanyia vitendo vya kikatili ikiwemo kuwadhalilisha kwa kuwavua nguo watuhumiwa wanaoshukiwa kujihusisha na vitendo vya kihalifu bila kuwafikisha kwenye vyombo vya dola jambo ambalo ni kinyume cha sheria, kanuni na taratibu za nchi,” alifafanua msemaji wa Polisi.
Alisema takwimu zinaonesha wazi kwamba tabia hiyo inaendelea kujengeka na kuonekana kwamba ni jambo la kawaida, lakini ni ukiukwaji mkubwa wa taratibu na sheria za nchi.
Bulimba alisema makamanda wote wa polisi nchini wameagizwa kufanya ukamataji wa watu wote wanaojihusisha na vitendo vya kihalifu kwa kisingizio cha hasira kali na kuwafikisha mahakamani kwa sababu watu hao kwa mujibu wa sheria, tayari wanakuwa wametenda kosa la jinai.