Waziri wa ulinzi wa Korea ya Kusini, Kim Tae-young, amejiuzulu, siku mbili baada ya wanajeshi wa Korea ya Kaskazini kukishambulia kwa makombora kisiwa kimoja cha nchi yake.
Barua yake ya kujiuzulu imekubaliwa na Rais Lee Myung-bak.
Bw Kim alilaumiwa na baadhi ya watu kwa kutochukua hatua za kutosha kujibu mashambulio yaliyofanywa na Korea ya Kaskazini.
Korea ya Kusini sasa imetangaza kwamba inabadilisha baadhi ya utaratibu wake wa kijeshi, na vile vile kuongeza idadi ya vikosi katika kisiwa ambacho kilishambuliwa.
Hayo yakiendelea, Uchina imeelezea wasiwasi wake kutokana na ushirikiano wa shughuli ya kijeshi kati ya Korea ya Kusini na Marekani, kufanyika mwishoni mwa wiki hii.