MFUGAJI aliyeua polisi kwa mkuki wa kichwa, Hango Masanja (19) amefariki dunia usiku wa kuamkia jana, baada ya kuvuja damu nyingi kutokana na majeraha ya risasi sehemu zake za siri.

Masanja anadaiwa alimpiga mkuki wa kichwa Sajenti Elikana Jumatano wiki hii, wakati polisi huyo na wenzake watatu walipokwenda kukutana na wafugaji waliokuwa wakituhumiwa kuvamia Kijiji cha Mfinga wakiambatana na maofisa wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga kutafuta suluhu kati ya wafugaji hao na wanakijiji.


Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Sadun Kabuma alisema kuwa Masanja aliyekuwa amelazwa wodi namba tatu katika hospitali hiyo, alifariki saa saba usiku wa kuamkia jana kutokana na majerahamakubwa aliyopata mwilini mwake.


Inadaiwa Sajenti Elikana baada ya kupigwa mkuki , polisi wanzake watatu waliokuwa wameambata naye katika kujihami walifyatua risasi na kujeruhi baadhi ya wananchi, akiwemo Masanja.


Dk. Kabuma alisema, Masanja alipata majeraha makubwa sehemu ya makalio upande wa kushoto na sehemu zake za siri ziliharibika vibaya baada risasi kupiga maeneo hayo.


“Ni kweli tulimpokea mgonjwa huyo akiwa amepigwa risasi makalio ya kushoto na kusambaza kabisa sehemu za siri… kitabibu nathibitisha kuwa kifo chake kimesababishwa na kuvuja kwa damu nyingi mwilini,” alisema Dk. Kabuma.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Isuto Mantage alisema Masanja ni miongoni mwa watuhumiwa wanne waliokamatwa katika msakounaendelea katika Kijiji cha Mfinga wilayani Sumbawanga ili kubainiwaliohusika katika mauaji ya polisi huyo.


Kamanda Mantage alisema watuhumiwa wengine watatu, mmoja kati yao anaendelea na matibabu katika hospitali hiyo huku wengine wakihojiwa, watafikishwa mahakamani mara baada ya uchunguzi wa awali kukamilika.