Magoli yenye utata kutoka kwa Frank Lampard na Salomon Kalou, yamefufua matumaini ya Chelsea kutetea ubingwa wao baada ya kuifunga Tottenham Hotspurs.
Sandro aliipatia Spurs bao lake baada ya kuachia shuti kali lililompita kipa Petr Cech katika dakika ya 19.
Kipa wa Spurs, Heurelho Gomes alitema shuti la Frank Lampard katika dakika ya 45, na akauzuia mpira usivuke mstari, lakini mwamuzi akapiga kipenga cha kuashiria goli.
Salomon Kalou alionekana kuzidi wakati akifunga bao la pili.
Hata hivyo Chelsea hawatojali utata huo, kwani ushindi wao umekata tofauti ya pointi hadi tatu na Man United, ambao wanacheza na Arsenal Jumapili.
Chelsea na United watakutana wiki ijayo Old Trafford, katika mchezo ambao huenda ukaamua bingwa wa msimu huu.