Kesi ya uhujumu chumi , kusafirisha na kuuza nje ya nchi aina 14 za wanyama hai 136, imeendelea kupigwa kalenda katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kilimanjaro kutokana na upelelezi kutokamilika.
Mbele ya Hakimu wa Mahakama hiyo, Ruth Mkisi, Wakili wa Serikali, Stella Majaliwa, alidai jana kuwa upelelezi wa kesi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.
Kesi hiyo ambayo ipo mbele ya Hakimu Mfawidhi, Simoni Kobelo, lakini ikatajwa mbele ya Mkisi inatarajiwa kutajwa tena Novemba 8, mwaka huu.
Washtakiwa katika kesi hiyo namba 04 ya mwaka huu ni mfanyabiashara ambaye ni raia wa Pakstani, Kamrani Ahmed, anayeishi mkoani Arusha; Hawa Mang’unyuka, ambaye nimfanyabiashara; Martin Kimati, Afisa Mifugo; raia wa Kenya, Jane Mbogo ambaye ni mfanyakazi wa KIA;Veronica Beno, Afisa Mkuu wa Usalama; na Locken Kimaro ambaye ni Afisa Usalama wa Kampuni inayosimamia uwanja huo ya Kilimanjaro Development Company Limited (KADCO).
Wanyama wanaodaiwa kutoroshewa nje ya nchi ni wenye thamani ya Dola za Marekani 113,715.00 (Sh. 170,572,500.00), mali ya Serikali ya Tanzania,ambapo walipandishwa mahakamani kwa mara ya kwanza Juni 10, mwaka huu.
Wanyama wanaodaiwa kusafirishwa kwenda Doha nchini Qatar ni twiga, pofu, digidigi, swala, paa, tai na ndege wa aina mbalimbali ambao walisafirishwa kabla au baada ya Novemba 26, mwaka jana