Na Shakoor Jongo
WASANII wapatao 20 wa tasnia ya filamu Bongo, juzikati walipata ajali mbaya baada ya gari aina ya Toyota Coaster walilokuwa wakisafiria kuchomoka tairi mbili za nyuma upande wa kushoto na kulifanya lipoteze muelekeo.
Tukio hilo lilitokea Januari 26, mwaka huu nje kidogo ya Wilaya ya Nzega wakati wasanii hao walipokuwa wakitoka Musoma mkoani Mara walikokuwa wamekwenda kurekodi filamu.
Akizungumza na chanzo hiki mara baada ya ajali hiyo kutokea, mmoja wa wasanii waliokuwa kwenye msafara huo, Steven Mengere ‘Steve Nyerere’ alisema: “Kwa kweli ni Mungu tu, yaani sasa hivi tungekuwa tunaongea mengine.
“Tulianza safari yetu vizuri baada ya kutoka katika Kijiji cha Butiama tulikoenda kushuti filamu yetu ya Nyerere Respect ndani ya gari kukiwa na wasanii kama ishirini na dereva, tulipofika maeneo flani nje kidogo ya Wilaya ya Nzega, tairi mbili za nyuma zikachomoka na kulifanya gari lipoteze muelekeo.


“Ilikuwa balaa, dereva alijitahidi sana kuokoa uhai wetu na baada ya mwendo mfupi likasimama. Baadhi ya wasanii waliumia kufuatia kujigonga kwenye machuma ila Bi Mwenda alikuwa hoi kwa presha,” alisema Steve.
Aliwataja wasanii walionusurika kifo katika ajali hiyo kuwa ni pamoja na Ruth Suka ‘Mainda’, Halima Yahya ‘Davina’ Heriethy Chumila, Mohammed Fungafunga ‘Jengua’, Juma Chikoka ‘Chopa’, Mzee Korongo, Anitha wa Matonya, Fatuma Makongoro ‘Bi Mwenda, Mzee Mbembe, Rahel Haule ‘Recho’, Farid Uwezo na wengineo.