Jumuiya ya Wawekezaji katika sekta ya Utalii Zanzibar (Zati) imesema imeshangazwa na serikali kushindwa kuyapatia ufumbuzi matatizo ukosefu wa huduma ya maji na umeme tangu kuanzishwa kwa sekta hiyo mwaka 1993.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Abdul Samad, alipokuwa akitoa taarifa ya Zati katika hafla ya chakula cha usiku kwa wanachama wa jumuiya hiyo iliyofanyika Mazizini mjini Zanzibar jana.
Alisema wawekezaji vitega uchumni wamekuwa wakitekeleza majukumu yao katika mazingira magumu kutokana na kukosekana kwa huduma ya maji safi katika miradi yao.
Samad alisema hoteli za kitalii zilizojengwa katika ukanda wa mashariki mwa Zanzibar, zinakabiliwa na tatizo la ukosefu wa maji na kutumia gharama kubwa kupata huduma hiyo.
Aidha, alisema pia ukosefu wa huduma ya umeme wa uhakika katika miradi ya utalii imekuwa ni kero kwa wawekezaji vitenga uchumi na kuomba serikali kuchukua hatua za dharura kuondoa tatizo hilo.
Alisema wanapata wasiwasi na uwezo wa utendaji wa viongozi katika Shirika la Umeme Zanzibar (Zeco) na Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) kutokana na kushidwa kutatua matatizo hayo licha ya sekta hiyo kuwa na mchango mkubwa katika pato la Taifa.
 
“Tumekuwa tukifanya vikao vya pamoja na mamlka hizo kila mara lakini wenzetu wameshindwa kuonyesha nia ya kuondoa matatizo hayo," alisema Samad huku akipigiwa makofi na wawekezaji hao.
Alisema huduma ya maji na umeme katika sekta ya utalii ina umuhimu mkubwa katika kuendeleza sekta ya utalii lakini imekuwa haipatikani na kuwavunja moyo wawekezaji.
“Hatuwezi kuendelea kujenga au kuimarisha sekta ya utalii na kufikia malengo bila ya kuwa na maji na umeme wa uhakika pamoja na mafuta ya dizeli na petroli,” alisema.