Sudan Kusini inasema kuwa imepewa mkopo na Uchina wa dola bilioni 8, kugharimia miradi kadha ya miundo mbinu.
Ikiwa utatekelezwa, mkopo huo utazidisha bajeti ya Sudan Kusini zaidi ya mara dufu.

Msemaji wa serikali mjini Juba, alieleza kuwa fedha hizo zitatumiwa kujenga barabara, daraja na mitandao ya simu, pamoja na kuendeleza kilimo na vinu vya nishati kwenye mito.

Hakutaja mpango wa kujenga bomba la mafuta hadi Bahari ya Hindi.

Uchina inanunua mafuta mengi ya Sudan Kusini, na inataka kubaki na uhusiano mwema na Sudan, mshirika wake wa miaka mingi, na Sudan Kusini, ambayo ilipata uhuru mwaka jana.