Serikali ya Sudan imesema zaidi ya raia wa Sudan kusini 12,000 wanapaswa kuondoka nchini humo katika kipindi cha wiki moja.

Gavana wa jimbo la White Nile,Yusuf -shabali, amesema kuwepo kwa raia hao katika eneo la Sudan kunasababisha tisho la usalama na la kimazingira.
Amewapatia raia hao wa kusini muda wa wiki moja kuondoka.

Sudan na Sudan kusini zimekuwa zikizozania eneo la mpaka baina ya nchi hizo, lenye utajiri wa mafuta wiki kadhaa za hivi karibuni.

Bwana Al-Shambali amesema serikali ya Sudan Kusini ilikubali kuwahamisha raia wake, zaidi ya mwaka mmoja uliopita.

Wengi wa raia hao wa kusini walihamia Kaskazini punde baada ya mkataba wa mwaka wa 2002, ili kutafuta ajira.

Maelfu ya raia hao kwa sasa wako jiani kuelekea nyumbani, lakini wamekwama katika mto wa Port Kosti karibu na mpaka na Sudan Kusini.

Serikali ya Khartoum imekataa kuwapa kibali cha kuiwezesha serikali ya Sudan Kusini iwavukisha ili waweze kuingia nchini mwao.

Serikali ya Sudan imekataa kuwapa kibali cha kurudi hadi ipate hakikisho kutoka kwa Sudan Kusini kuwa haitatumia vibali hivyo kupitisha vifaa vya kijeshi na wapiganaji nchini Sudan.