Sifael Paul na Intaneti
USIKU wa Jumapili iliyopita ‘kichaa’ wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul ‘Diamond’ alijitengenezea historia nyingine duniani baada ya kuangusha bonge la shoo ndani ya mjengo wa Big Brother Africa ‘StarGame’ jijini Johannesburg, Afrika Kusini na kupewa jina la R.Kelly (Robert Kelly) wa Tanzania.
Kupitia runinga na mitandao mingi ya kijamii, nchi mbalimbali duniani zilimshuhudia Diamond akitoa burudani ambayo ilimfanya mkuu wa mjengo huo, Big Brother kumpigia saluti na kumpa jina la R.Kelly wa Tanzania.
Wimbo uliotikisa mjengoni humo ni Mawazo ambao ulisababisha Big Brother kushindwa kuamini kwani ilikuwa ni zaidi ya matarajio ya wengi.
Mwisho wa shoo hiyo iliyomfanya Diamond sasa kuwa staa wa dunia, Big Brother alikiri kuwa msanii huyo ni kijana mdogo wa Tanzania ambaye alifanya poa sana usiku huo.
Muda mfupi baada ya shoo, Diamond aliyekuwa aking’aa na pamba zilizobuniwa na Kidoti akiwa amevalia suruali nyekundu, shati nyeupe, koti jeusi na tai nyekundu, aliandika kwenye kurasa zake za Mitandao ya Kijamii ya Twitter na Facebook:
“Watanzania wenzangu bila ninyi mimi si kitu. Nawashukuru sana kwa maombi yenu, pia namshukuru mama yangu mzazi (Sandra) na wote mnaonisapoti. One Love!”
Kwa mujibu wa maoni ya watu kutoka nchi mbalimbali duniani, shoo ya Diamond ilikuwa ni balaa huku kila mmoja akiomba atembelee nchini kwao.
“Muda si mrefu natarajia atakuja huku Nigeria, tunamsubiri kwa shauku kubwa,” yalisomema maoni ya Suzzy wa Nigeria huku yakiungwa mkono na watu wa nchi nyingine.