MKAZI wa Kijiji cha Kilombero, mkoani Geita, Mahangaiko Buruhe (52) amefariki dunia baada ya kusombwa na upepo mkali ulioambatana na mvua wakati akijaribu kuzuia nyumba yake isianguke.

Tukio hilo lilitokea juzi saa 10;00 jioni ambapo marehemu alikuwa akizuia nyumba yake isisombwe na upepo baada ya kushuhudia paa la nyumba likiezuliwa na upepo.
Marehemu aliamua kurukia kenchi ili kuzua nyumba isianguke kwa kutumia nguvu zake na kwamba upepo ulimzidi nguvu, paa likaezuliwa na marehemu kurushwa nje na kuangukia nyumba ya pili alikopoteza maisha.

Mashuhuda wa tukio hilo Makwiwa Bihalale (mke wa marehemu) na Chausiku Malole walisema marehemu alikuwa akifanya juhudi za kuokoa nyumba isianguke na upepo ndipo mauti yakamkuta hali ambayo imewashtua.
Akizungumza mbele ya viongozi waliotembelea hapo kuona tukio hilo, Kaimu Ofisa Tarafa ya Busanda, Joseph Kaparatus alisema tukio hilo lilitokana na ujenzi mbovu wa nyumba hiyo na kwamba iliezekwa bila kuzingatia utaalamu na haina kenchi zaidi ya mbao ambazo zimegongelewa bati.
“Nyumba hii ilikuwa na uhalali wa kuanguka mkuu, angalia haijajengwa kwa kuzingatia utaalamu wa ujenzi wa nyumba,” alisema Kaparatus.

Awali akizungumza na wakazi wa eneo hilo nyumbani kwa marehemu Mkuu wa Wilaya ya Geita, Said Mangochie aliwataka wanachi hao kujenga nyumba bora zinazozingatia utaalamu ili kuepusha majanga wakati wa mvua.

Mwenyekiti wa kijiji hicho Haruna Shabani alisema marehemu aliwahi kuwa mtendaji wa kijiji, na kiongozi wa CCM Kata ya Busanda, ameacha wajane wawili na watoto 18.