UZEMBE wa Wauguzi wa Wodi ya Wazazi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kuchelewa kumpokea na kumpa huduma zinazostahili mjamzito, kumesababisha  kujifungua hadharani nje ya wodi.
Mama huyo aliyefahamika kwa jina la Tausi Saidi (29), mkazi wa Mbete katika Manispaa ya Morogoro, alifikishwa hospitalini hapo na  muuguzi wa Zahanati ya Mbete iliyopo Kata ya Mlimani akiwa ameambatana na ndugu zake  Januari 7, saa 10 jioni akiwa anaumwa uchungu.
Kwa mujibu wa mume wa mwanamke huyo, Kudra Khalfani alisema kwamba mke wake alianza kupata uchungu na hivyo kumpeleka Zahanati ya Mbete. Baada ya kufika huko, alilazimika kupelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro baada ya kuonyesha dalili za kujifungua
Alisema baada ya kufika wodi ya wazazi, nesi waliyeambatana naye aliyemtaja kwa jina moja la Mwacha, aliingia wodini na kumtaka nesi wa wodi hiyo kwenda kumwangalia mgonjwa wito ambao alidai haukuitikiwa na muuguzi huyo.
Mwanaume huyo alisema katika hali isiyokuwa ya kawaida, muuguzi huyo aliwataka kumpeleka mama huyo wodi namba saba ‘B’ bila kutoa msaada wowote  ikiwa ni pamoja na kujua hali ya mgonjwa.
“Baada ya nesi kukataa kumpokea mke wangu, kwa kuwa alikuwa hawezi hata kutembea ilibidi nisaidiwe na watu wanne  kisha tukambeba mikononi, kwa kuwa hata kitanda cha kumbebea hatukupewa, na kabla ya kufika akasema tumshushe akawa amejifungulia koridoni na mtoto haikuwa riziki yetu” alisema.
“Imeniuma sana mwanamke mwenzetu amedhalilishwa sana, huwezi kuamini amejifungulia korido watu wote wanamwangalia. Sijapenda hali kama hii inatakiwa ikomeshwe kwani kulikuwa na sababu gani ya kumfanya nesi wa wodi ya wazazi kushindwa kumsaidia huyu mama,” alisema Mwajuma Ally.
Hata hivyo alisema mimba ya mwanamke huyo ilikuwa haijafikisha umri wa kujifungua, kwamba alishawahi kupoteza mimba nne na kwamba ana matatizo katika suala la uzazi.
“Hata mimba hii iliyotoka tayari alishakuwa na vidokezo vya hatari na aliambiwa asifanye kazi ngumu, lakini inaonekana alikuwa anafanya kazi ngumu.
Aliongeza kuwa pamoja na kupewa hiyo tahadhari katika kadi yake ya kliniki, ilionyesha kuwa amehudhuria kliniki mara moja tu.
Kuhusu mwili wa kichanga hicho, mganga mkuu huyo alisema ndugu wamegoma kuukabidhi kwa uongozi wa hospitali hiyo kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kidaktari.
Aidha, mmoja wa ndugu zake, Shida Said alipoulizwa sababu ya kukataa kuukabidhi mwili wa kichanga hicho  alisema hakuna sababu ya kuwapa mwili huo kwa kuwa walishindwa kumsaidia mgonjwa wao.