Kuna taarifa za kutatanisha kuhusu operesheni iliyofanywa na Ufaransa ili kumkomboa mateka mmoja anayezuwiliwa na wapiganaji wa al-Shabaab nchini Somalia.Msemaji wa kundi hilo la wapiganaji alieleza kuwa operesheni hiyo iliyofanywa Ijumaa usiku na makamando haikufanikiwa, na kwamba Mfaransa mmoja amekufa.
Serikali ya Ufaransa haikusema kitu kuhusu operesheni yao hiyo ya jana usiku ambayo inaonesha ilifanywa na makamando ambao walipelekwa kusini mwa Somalia kwa helikopta.
Msemaji wa al-Shabaab amearifu kuwa operesheni hiyo ilishindwa na kuna taarifa kuwa mzungu mmoja amekufa kwenye tukio hilo.
Tovuti moja mashuhuri ya habari nchini Ufaransa inaarifu kuwa habusu mwenyewe, askari wa ujasusi wa Ufaransa aliyetekwa mwaka wa 2009 ameuwawa, lakini taarifa hizo hazikuthibitishwa.
Inavoelekea operesheni hiyo inahusiana na Ufaransa kuamua kuingilia kati kijeshi nchini Mali - uamuzi ambao serikali inatambua kuwa utaathiri piya hali ya mateka 9 wa Ufaransa wanaozuwiliwa sehemu mbali-mbali za Afrika.