Waziri Mkuu mizengo Pinda 
Dar es Salaam.
 Tume ya Kuchunguza Matokeo ya Kidato cha Nne mwaka 2012, imeanza kazi kwa kuwahoji walimu, wanafunzi na wajumbe wa bodi za shule kuhusu sababu za matokeo mabaya.
Mwenyekiti wa tume hiyo Profesa Sifuni Mchome, alisema jana kwamba shughuli hiyo imeanza katika Kanda ya Dar es Salaam ambapo wajumbe watatembelea shule 12.

“Tumeamua kuzungumza na wanafunzi waliopo shuleni na wale waliofanya mtihani huo watakaopatikana ili kujua ni nini kilichofanya wakapata alama hizo, pia itakuwa njia rahisi ya kupata watu wengi ikiwa ni pamoja na bodi za shule,” alisema Profesa Mchome:
“Kazi kwa Dar es Salaam ilianza Jumatatu na itaisha Ijumaa, kuna shule ambazo zimeainishwa. Tukifika kwenye hizo shule na kama zipo shule zingine jirani tutawaita waje kutoa maoni yao.” alisema.

Profesa Mchome alisema kuwa, ili kufanikisha shughuli hiyo wameteua kanda tano ikiwamo ya Dar es Salaam, Kusini, Mashariki, Kati na Kanda ya Magharibi ambayo itahusisha Mikoa ya Geita na Simiyu.

Profesa Mchome alieleza kuwa, ili kupata maoni ya wananchi wengi wamefungua tovuti inayoitwa www.tumek4.go.tz ili wengine watoe maoni huko.

Alisema kuwa, kanda hizo zimetengwa kwa kuzingatia hadidu za rejea zilizotolewa na Waziri Mkuu, ambapo wamechangua shule zilizofanya vibaya, zilizokuwa na ufaulu wa kati na zilizofanya vizuri ambazo ni zile za Serikali na zisizo za Serikali.

Alisema kuwa, tayari wameshazungumza na maofisa elimu pamoja na Muungano wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (Tahosa).

Alisema kuwa, baada ya kutembelea shule hizo Dar es Salaam, juma lijalo timu hiyo itaenda katika kanda nyingine ambapo zitatembelewa shule 13.

Alisema kuwa, leo ratiba ya shughuli ya tume hiyo itawekwa katika tovuti yao.Profesa mchimo aliwataka wananchi watoe zaidi maoni yao kupitia tovuti hiyo, pamoja na vyombo vya habari ili waweze kukamilisha shughuli hiyo kwa kupata maoni ya watu wengi.