Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Wilbrod Slaa akizungumza  na waandishi wa habari  Dar es Salaam jana. Kulia ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu. Picha na Rafael Lubava                            
Mvutano uliopo hivi sasa kati ya Chadema na Bunge ulianza Februari 4 katika kikao cha Bunge mjini Dodoma baada ya wabunge wa Chadema kupinga msimamo wa kiti cha Spika wakieleza unapendelea

Boniface Meena na Mussa Juma, Mwananchi
Kutokana na mvutano ambao umekuwapo mara kwa mara kati ya Chadema na Spika wa Bunge, Anne Makinda, chama hicho kimemkumbuka aliyekuwa Spika wa Bunge la 10, Samuel Sitta kikieleza kuwa alikuwa hapindishi sheria na kanuni za Bunge na ndiyo maana lilikuwa limetulia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana kuhusu wabunge wa chama hicho kutakiwa kuhojiwa na Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema Spika Makinda amekuwa akipindisha kanuni na ndiyo maana kumekuwa hakuna utulivu bungeni.

“Spika Sitta aliyekuwepo kabla ya Makinda alikuwa hapindishi sheria na alikuwa anajirekebisha pale anapokosea na tulikuwa tukishauriana kwamba asijihusishe na mambo ya vyama,” alisema Dk Slaa.

Alisema Sitta, ambaye hivi sasa ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alikuwa hafuati mambo ya vyama kwa kuwa alitakiwa kuwa ni mtu ambaye hapendelei upande wowote. Sitta, ambaye alikuwa Spika kuanzia mwaka 2005-2010, alikuwa anajinadi kwa kuendesha Bunge kwa spidi na viwango.

“Makinda aachane na ushabiki wa CCM kwani anajua kabisa kanuni ya nane inamtaka Spika asifungamane na upande wowote hivyo aache kufanya hivyo,” alisema Dk Slaa.

Alisema ni muhimu Spika akawaeleza kimaandishi amepata wapi mamlaka ya kuruhusu kamati iendelee wakati zote zilivunjika rasmi katika Bunge lililopita.
“Spika kama hajui kanuni aende shule kujifunza kuliko kututia aibu, wanasheria, wabunge wamsaidie ili aweze kuelewa.”

Dk Slaa alisema katika mabunge ya kidemokrasia, kupongeza ni jambo halali na kuzomea pia ni jambo halali hivyo kitendo cha wabunge wao kuzomea ni sawa kwa kuwa ni njia yao ya kufikisha ujumbe. Akizungumzia suala la wabunge wake kuhojiwa na kamati hiyo ya Bunge, alisema hawatakwenda kuhojiwa na kamati hiyo na kama Bunge litaamua kuwafukuza lifanye hivyo ili wananchi waelewe.

“Hawawezi kwenda kuhojiwa na kamati ambayo haipo kisheria, nilipokuwepo bungeni nilishiriki kuandaa kanuni hizi za Bunge, Spika hana mamlaka anayojipa ya kuongeza muda wa kamati, hivyo aache kulidhoofisha Bunge na badala yake alisaidie,” alisema Dk Slaa.

Akizungumzia suala hilo, Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu alisema anashangazwa na Naibu Spika, Job Ndugai kusema kuwa kuna kamati ambazo huwa zinaendelea wakati nyingine zinapokuwa zimemaliza muda wake.

Lema aitisha maandamano
Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema, ametangaza kuandaa maandamano makubwa yatakayoshirikisha wanawake na watoto katika Jiji la Arusha ili kushinikiza Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Arusha (AUWSA) kuwasambazia maji.

Akizungumza jana, Lema alisema ameamua kuandaa maandamano hayo ya kudai maji kwani kwa zaidi ya miezi sita sasa asilimia 70 ya wakazi wa Jiji la Arusha hawapati maji safi.

“Nimewaandikia barua AUWSA wiki mbili sasa nikiwataka wanipe mipango yao ya muda mfupi na mrefu ya kuondoa tatizo la maji Arusha, kwani mimi kama mbunge ninaweza kushirikiana nao kupunguza tatizo hili, lakini hawajajibu sasa tutawashinikiza kwa nguvu wa umma,” alisema Lema.