Salva Kiir(r), Sudan Kusini na Omar Bashir, Sudan(l).
Serikali za Sudan na Sudan kusini zimesaini mkataba mpya wa kurejelea uchimbaji na usafirishaji wa mafuta kutoka Sudan Kusini kupitia mabomba ya Khartoum.
Mkataba huu unakomesha mzozo uliokuwa kati ya nchi hizo mbili kwa muda wa mwaka mzima. Serikali ya Juba ilikatiza uchimbaji mafuta Januari mwaka uliopita kufutia mtafaruku juu ya ada zinazotozwa.
Waziri wa habari wa Sudan ya kusini Barnaba Marila Benjamin, ameambia BBC kuwa nchi hizo zimeafikiana na kusaini mkataba juu ya ugawaji wa fedha za mafuta kufuatia upatanishi ulioongozwa na rais wa zamani wa Afrika Kusini Thabo Mbeki.
Nchi hizo mbili zilitishia kuingia vitani kutokana na mvutano hasa juu ya mafuta na mipaka tangu Sudan ya Kusini ijitenge kuwa huru mwaka wa 2011.