Nairobi.
 Uhuru Kenyatta jana aliapishwa kuwa Rais wa Nne wa Jamhuri ya Kenya, huku akiahidi kutilia mkazo kudumisha amani na umoja.

Akihutubia halaiki ya Wakenya walihudhuria hafla hiyo kwenye Uwanja wa Michezo wa Moi, Kasarani wakiwamo wakuu wa nchi na wawakilishi wa Serikali mbalimbali za kigeni, Rais Uhuru alisema ataongoza kwa haki kwa kuwapa nafasi waliomchagua na ambao hawakumpigia kura.

Rais Kenyatta aliapishwa jana baada ya kushinda Uchaguzi Mkuu wa Kenya uliofanyika Machi 4, mwaka huu kwa kura 6,173,433 ikiwa niasilimia 50.51 ya kura 12,338,667 zilizopigwa. Raila Odinga, ambaye alikata rufaa kupinga matokeo hayo na kushindwa, alifuatia kwa kupata kura 5,340,546 sawa na asilimia 43.70.

“Amani na umoja havitadumishwa hivihivi tu, bali vitakuja kwa wananchi wote kupatiwa fursa sawa za kiuchumi,” alisema Kenyatta, ambaye pia alitumia nafasi hiyo kuwashukuru viongozi waliotangulia wa taifa hilo akiwamo baba yake, Jomo Kenyatta, Daniel arap Moi na Mwai Kibaki, ambaye alikabidhi madaraka jana.Kenyatta (51), ameweka rekodi ya kuwa Rais mdogo zaidi wa Kenya, pia aliwashukuru wapinzani wake kwa kushiriki kuimarisha demokrasia.

Nairobi yalipuka kwa furaha
Shangwe, hoihoi, vifijo na nderemo vilisikika wakati Kenyatta alipokuwa akiapishwa akiwa na mkewe.


“Ninaapa kuwa nitakuwa mwaminifu na mtiifu kwa Katiba ya Kenya,” alisema Kenyatta huku akiwa ameshika kitabu kitakatifu cha Biblia wakati akila kiapo.


Ilielezwa awali kuwa mkewe ndiye ambaye angemshikia Biblia wakati wa kuapishwa, lakini hali haikuwa hivyo kwani aliishika mwenyewe. Pia Naibu Rais, William Ruto naye aliapishwa wakati wa shughuli hiyo.


Hafla hiyo, iliyosusiwa na Odinga, ilihudhuriwa na Rais Jakaya Kikwete. Viongozi wengine waliohudhuria ni pamoja na Rais Yoweri Museveni, (Uganda), Salva Kiir (Sudan Kusini), Hassan Sheikh Mohamud ( Somalia), Jacob Zuma (Afrika Kusini), Ali Bongo (Gabon), Jonathan Goodluck (Nigeria) na Joseph Kabila wa DRC.


Wengine ni Paul Kagame (Rwanda), Ismail Guelleh (Djibouti), Robert Mugabe (Zimbabwe), Haile Mariam Desalegn (Ethiopia), Rais mstaafu wa Kenya, Moi na Kenneth Kaunda wa Zambia.


Msajili wa Mahakama Kuu, Gladys Boss Shollei ndiye alimwapisha Kenyatta huku Jaji Mkuu, William Mutunga akishuhudia.

Museveni ang’aka
Akizungumza katika hafla hiyo Rais Museveni alipongeza ujasiri wa Wakenya kumchagua Kenyatta licha ya kukabiliwa na mashtaka kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC).
Kenyatta na Ruto wanakabiliwa na mashtaka ICC, yenye makao makuu huko The Hague, Uholanzi.Wanatuhumiwa kwa kuhusika katika ghasia za kikabila zilizotokea baada ya Uchaguzi Mkuu wa Kenya wa mwaka 2007 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 1,100 huku maelfu wakilazimika kuyakimbia makazi yao.
Kenyatta na Ruto, ambao wamekana tuhuma hizo wamekubali kushirikiana na ICC.