Rais wa Marekani, Barack Obama imeidhinisha mpango wake wa kutoa ufadhili wa kijeshi kwa Somalia wakati nchi hiyo ikiendelea kujijenga upya kufuatia miaka mingi ya mzozo.

Bwana Obama, alitoa ujumbe huo kwa waziri wa mambo ya nje John Kerry, akisema kuwa hatua hiyo italeta usalama na kukuza amani.
Hatua hiyo sasa hivi inatoa nafasi kwa Kerry kutoa msaada wa kijeshi kwa Somalia.

Mwezi jana baraza la usalama la Umoja wa Mataifa, lilikubali kuondoa kwa muda marufuku ya kuuza silaha kwa Somalia kwa mwaka mmoja.

Uamuzi unaruhusu serikali ya Somalia, kununua silaha nyepesi ili kuisaidia kupambana na makundi ya wapiganaji wa Al Shabaab.

Na nchi kadhaa, zilikuwa zinasuasua kuhusu kulegeza marufuku hiyo kwa hofu ya kuchochea utovu wa usalama Somalia.

Lakini kwa kuondoa marufuku hiyo, iliyowekwa mwaka 1992 ilikuwa kazi ngumu ya shinikizo kutoka kwa rais wa serikali mpya Hassan Sheikh Mohamud.

Marekani ilitambua rasmi, Somalia mwezi Januari hususan kutambua maendeleo ya serikali mpya katika kuleta uthabiti wa nchi na juhudi zao kutaka kumaliza harakati za al-Shabab.

Marekani haikuwahi kusitisha uhusiano na Somalia lakini mwaka 1993 wakati wanajeshi wake 18, waliuawa baada ya wapiganaji wa Somalia kupiga risasi ndege mbili za kijeshi angani na huo ndio ulikuwa mwanzo wa nchi hiyo kuanza kutumbukia katika mgogoro wa kisiasa.

Rais Mohamud, alichukua mamlaka mwaka 2012 baada ya uchaguzi wa kwanza wa aina yake, tangu kuondolewa mamlakani kwa Mohamed Siad Barre mwaka 1991.